CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimetangaza maandamano ya amani bila kikomo nchi nzima, hadi pale Serikali itakapofanyia kazi maoni na mapendekezo ya wadau kuhusu upatikanaji katiba mpya na chaguzi huru na za haki. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Maandamano hayo yametangazwa leo tarehe 13 Januari 2024 na Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe, wakati anazindua rasmi vuguvu la kudai haki Tanzania katika ofisi mpya za chama hicho, jijini Dar es Salaam.
Mbowe amesema maandamano hayo yataanzia jijini Dar es Salaam, tarehe 24 Januari mwaka huu, hadi pale Serikali itakapondoa miswada hiyo bungeni jijini Dodoma.
“Chama kinatangaza maandamano ya amani kuishinikiza Serikali kuzingatia maoni na mapendekezo ya wadau mbalimbali wa uchaguzi nchini ambayo yataanza tarehe 24 Januari siku ya jumatano na kuendelea mikoani kwa kadri itakavyopangwa hadi hapo Serikali itakapondoa miswada hiyo na kusikiliza na kuheshimu maoni ya watanzania,” amesema Mbowe.
Mbowe amesema uamuzi huo ni matokeo ya kikao cha kamati kuu ya Chadema kilichofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 8 Januari mwaka huu kwa ajili ya kujadili miswada ya uchaguzi iliyowasilishwa bungeni jijini Dodoma.
Masuala mengine yaliyojadiliwa ni ugumu wa maisha na uamuzi wa Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kutofanyia kazi maoni ya wadau kuhusu marekebisho ya mfumo wa demokrasia ya vyama vingi, hususan mifumo ya chaguzi ili iwe huru na haki, yaliyotolewa na wadau kupitia Kikosi Kazi kilichoundwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.
“Jambo la kusikitisha mapendekezo yaliyowasilishwa kwa Rais na wao walikuwa wadau na washiriki ndani ya kikosi lakini mawazo yote yalipuuzwa. Tangu mfumo wa vyama vingi vya siasa kwenye chaguzi zote waangalizi wa kimataifa na wa ndani wamekuwa wakionyesha mapungufu na kukosekana tume huru ya uchaguzi,”
“ Na wametoa mapendekezo mamhususi kwamba mfumo wetu wa uchaguzi hauko sawa na kila mtanzania utakayemuulizia kuhusu mfumo wa uchaguzi atakwambia chaguzi zetu haziko sawa, wametoa maoni yao kuhusu umuhimu wa tume huru ya uchaguzi ila kwenye miswada hii maoni hayo hayakutiliwa maanani,” amesema Mbowe.
Mbowe alidai, miswada iliyowaislishwa bungeni haikuzingatia maamuzi ya mahakama mbalimbali za kikanda ikiwemo Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Mahakama ya Afrika Mshariki, ambazo ziliamrisha sheria zirekebishwe ili kuondoa vifungu vinavyoagiza wakurugenzi wa halmashauri kuwa wasimamizi wa uchaguzi.
Mbowe amesema Kamati Kuu ya Chadema, inapendekeza Serikali iondoe bungeni jijini Dodoma miswada yote ya uchaguzi ili iandikwe upya kwa kuzingatia maoni ya wadau, pamoja na marekebisho ya mpito ya katiba yafanyike ili kuondoa dosari zitakazoathiri sheria zitakazotungwa.
Awali, Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika, alisema 2024 utakuwa mwaka wa mapambano ya uchaguzi na katiba mpya.
“Niliwaambia kwamba 2024 utakuwa pamoja na mambo mengine ni mwaka wa mapambano ya mabadiliko ya mwaka wa mapambanao ya uchaguzi,” amesema Mnyika.
Leave a comment