Waziri wa Madini, Anthony Mavunde amesema serikali itahakikisha inakuja na suluhisho la migogoro baina ya wachimbaji inayojitokeza katika eneo la machimbo ya madini ya Tanzanite ili kuchochea uzalishaji zaidi wa madini hayo ya vito. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Hayo yamesemwa leo Jumapili Mirerani mkoani Manyara na Mavunde wakati wa hafla ya kutoa tuzo kwa wachimbaji waliotekeleza mpango wa wajibu kampuni kwa jamii (CSR) kwa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro, mkoani Manyara.
“Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan imerusha ndege nyuki ndani na nje ya ukuta wa Mirerani kubaini viashiria vya mwamba wa madini hatua ambayo itapelekea wachimbaji wengi kuchimba kwa uhakika.
Kupitia utaratibu huu wa kupata viashiria vya mwamba wa madini itasaidia kutatua changamoto ya mtobozano chini ya ardhi kwa wachimbaji wengi kujikuta eneo moja la uchimbaji na hivyo kupelekea migogoro miongoni mwao.
“Ninawapongeza wachimbaji wote mliorudisha kwa jamii kwa kuboresha huduma za Afya na Elimu,niwaombe Halmashauri ya Wilaya kwa kushirikiana na Chama cha Wachimbaji Manyara(MAREMA) kuweka utaratibu mzuri zaidi ili kundi kubwa la wachimbaji liweze kuchangia huduma za msingi kwa jami,” alisema Mavunde
Akitoa salamu zake,Mbunge wa Jimbo la Simanjiro, Christopher Ole Sendeka (CCM) ameishukuru Serikali kwa kuendelea na ujenzi wa kituo cha Biashara ya Madini-Tanzanite Exchange Centre (TEC) ambacho kitachochea maendeleo na ukuaji wa kasi wa Mji wa Mirerani.
Akimkaribisha mgeni rasmi, mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga amewataka wamiliki wa leseni kuwa mstari wa mbele kuchochea maendeleo ya Jamii zinazonguka machimbo ya madini ili kuboresha huduma za msingi na kukuza uchumi wa jamii husika.
Leave a comment