Waziri wa Madini, Anthony Mavunde ameipongeza Kampuni ya Perseus kwa kufanikiwa kukamilisha wa mchakato wa ununuzi wa hisa za Kampuni ya Ore Corp na kuitaka kampuni hiyo kukamilisha haraka malipo ya fidia kwa wananchi wanaopisha mradi wa uchimbaji dhahabu wilayani Sengerema mkoani Mwanza. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Mavunde amebainisha hayo leo tarehe 19 Aprili alipofanya kikao cha pamoja na Kampuni ya Perseus ya Australia ikiongozwa na Mtendaji Mkuu wake, Jaffer Quartamaine.
Kikao hicho kilizungumzia uendelezwaji wa mradi wa Nyanzaga unaomilikiwa kwa ubia kati ya Serikali ya Tanzania na Kampuni ya Ore Corp ambayo hisa zake zimenunuliwa na Kampuni ya Perseus.
Pia amewataka wawekezaji hao kuhakikisha wanaanza mapema uendelezaji wa mradi kwa mujibu ya makubaliano ya awali ya kimkataba ili nchi ianze kunufaika na matunda ya utekelezaji wa mradi wa uchimbaji mkubwa wa madini dhahabu wa Nyanzaga uliopo Wilaya ya Sengerema mkoani Mwanza.
Akizungumza katika kikao hicho, Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Perseus, Jaffer Quartamaine ameishukuru serikali ya Tanzania kwa ushirikiano mkubwa wakati wote wa mchakato wa ununuzi wa hisa za Kampuni ya Ore Corp.
Pia ameahidi kwamba wamejipanga kuanza uendelezaji wa mradi huu mapema kadri iwezekanavyo kutokana na mpangilio wa utekelezaji wa shughuli mbalimbali za utekelezaji wa mradi.
Ameongeza pia kwamba wamejipanga kufanya uwekezaji mkubwa na wa mfano kwa kutumia teknolojia ya kisasa ili kuongeza uzalishaji wa dhahabu nchini.
Leave a comment