MWANACHAMA wa Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Boniface Jacob, amedai kuna baadhi ya vigogo serikalini wana mitandao ya uchotaji fedha katika mapato na miradi inayotekelezwa katika halmashauri, ndio maana vitendo vya ubadhirifu haviishi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Jacob ametoa madai hayo leo tarehe 19 Aprili 2024, jijini Dar es Salaam, akichambua ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere, kwa mwaka wa fedha wa 2022/23.
“Viongozi wa juu wanamtandao katika hizo halmashauri kwa maana hiyo ni wanufaika kidogo, kwa hiyo maana hiyo ni wanufaika kwenye huo ubadhirifu na kama sio wanufaika kwa nini hatuoni sababu hawakuchukua hatua kali na madhubuti ufisadi katika halmashauri zetu,” amesema Jacob.
Mwanasiasa huyo aliyewahi kuwa Meya katika Halmashauri za Manispaa ya Kinondoni na Ubungo, mkoani Dar es Salaam, amesema kila ripoti ya CAG inapotolewa na kuibua madudu, maoni yanatolewa juu ya namna ya kuyadhibiti ikiwemo kuwachukulia hatua wahusika.
“Nimetoa mfano mwaka jana na hii ni changamoto kubwa, wizi na ubadhirifu vinazidi kukua na havipungui lakini tunaongea na havifanyiwi kazi . Hela zinazoibiwa katika halmashauri zimeongezeka nashauri viongozi wa Serikali za mitaa wachukue hatua,” amesema Jacob.
Jacob amesema uchambuzi wake alioufanya katika ripoti hiyo umeonesha fedha kiasi cha Sh. 20.3 bilioni, zilizokusanywa na mamlaka za Serikali za mitaa kwa ajili ya kufanya miradi ya maendeleo hazikutolewa na kwamba zimeenda katika matumizi yao binafsi kama kulipana posho.
Jacob amesema ripoti ya CAG imebainisha fedha kiasi cha Sh. 19.7 bilioni, zilizopangwa kutekeleza miradi ya maendeleo hazikufanyiwa kazi kitendo kinachoweza sababisha kupigwa.
“Kuna wakati tunalalamika barabara mbovu wakati fedha zinabaki, CAG amesema malaka 27 za serikali za mitaa hazikuzitumia, zikisahaulika tukija tafuta tunaambiwa zinaliwa sababu zinakuwa kama chenji,” amesema Jacob.
Pia, Jacob amesema ripoti hiyo imebainisha fedha kiasi cha Sh. 28 bilioni zilitumika nje ya bajeti.
“katika taarifa hiyo CAG anasema amegundua kuna manunuzi yamefanyika bila ushindani ya kiasi cha Sh. 4.6 bilioni kwa nchi nzima kinyume na kanuni ya manunuzi ya umma,” amesema Jacob.
Leave a comment