MAKAMU wa Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassani ameahidi kusimamia ujenzi wa barabara ya Korogwe Vijijini hadi Tanga Mjini, ili kutekeleza ahadi aliyoitoa Rais John Magufuli na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa mkoani humo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Tanga…(endelea).
Ametoa ahadi hiyo leo tarehe 15 Machi 2021, katika ziara yake mkoani Tanga, baada ya Mbunge wa Korogwe Mjini, Dk. Alfred Kimea, kumuomba asimamie ahadi hiyo ili barabara hiyo ijengwe kwa kiwango cha lami.
Akijibu ombi hilo, Mama Samia amesema atawasiliana na Serikali ya Mkoa wa Tanga, ili kupanga namna ya upatikanaji wa fedha kwa ajili ya kuijenga.
“Sijasahau barabara iliyoombwa, kwamba imesemwa hapa ni ahadi ya Rais Magufuli, nitafuatilia na nitawasiliana na serikali ya mkoa kuona jinsi itakavyoombewa fedha na kuona jinsi inatimizwa,” ameahidi Mama Samia.
Akitoa mapendekezo hayo, Dk. Kimea amesema Rais Magufuli na Waziri Majaliwa, waliwaahidi watu wa wilaya ya Korogwe mkoani humo, kwamba barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami, ili kuwuanganisha wananchi wa Korogwe Vijijini, Korogwe Mjini, Mkinga na Tanga Mjini.
“Rais pamoja na waziri mkuu walituahidi watajujenge barabara ambayo ni tegemeo la watu wa Korogwe Mjini, Korogwe Vijijini , na watu wa Mkinga. Barabara inayotokea Korogwe- Mndolwa- Magoma na kuunganisha watu wa Tanga Mjini,” amesema Dk. Kimea na kuongeza:
“Mheshimiwa makamu wa rais tunaomba tuone namna gani tunaijenga kwa kiwango cha lami ili watu wa Korogwe Mjijini, Korogwe Vijijini na Mkinga waunganishwe.”
Mama Samia yuko ziarani mkoani Tanga kwa muda wa siku tano, kuanzia leo Jumatatu hadi Ijumaa ya tarehe 19 Machi 2021.
Leave a comment