NYANSOLOLI Paul, mkazi wa Kijiji cha Kishapu mkoani Shinyanga, anashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa tuhuma za kumuua kisha kumla mtoto wake wa kumzaa aliyekua na umri wa mwaka mmoja na miezi saba. Anaripoti Mwandishi Wetu, Shinyanga…(endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa hivi karibuni na Kamanda wa Jeshi la Polisi Shinyanga, Janeth Magomi, mtuhumiwa huyo anadaiwa kutenda tukio hilo tarehe 4 Januari mwaka huu, baada ya kuondoka naye nyumbani mtoto wake kisha kwenda katika mbuga za mashamba.
Kamanda Magomi alisema, tarehe 8 Januari 2024, mtuhumiwa huyo alirejea nyumbani bila mtoto baada ya wanafamilia kumhoji kwa nini hajarudi naye, alijibu kwamba amemla.
“Alirudi nyumbani akiwa hana mtoto, wanafamilia walipomhoji kwa nini hana mtoto alichokisema ni kwamba yeye amemla mtoto wake. Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Shinyanga alifika kwenye familia na kuanza uchunguzi wa tukio mara moja. Katika mahojiano alisema alimuua na kumla nyama mtoto huyo katika mbuga za mashamba,” alisema Kamanda Magomi.
Kamanda Magomi alisema upelelezi ulifanikisha kubaini fuvu la binadamu katika eneo linakodaiwa kufanyika tukio, kisha sampuli zake pamoja na za mtuhumiwa zilichukuliwa kwa ajili ya kufanyiwa vipimo vya DNA kubaini kama la mtoto wake.
“Ofisi ya Upelelezi Wilaya ya Shinyanga ilipeleka jalada ofisi ya mwanasheria wa serikali ambapo pia katika upelelezi mtuhimiwa alikwenda hospitali kupima kama akili yake iko sawa na tunaendelea kufuatilia upelelezi na taarifa za vinasaba kuthibitisha kama ni kweli mtoto wake,” alisema Kamanda Magomi.
Baadhi ya majirani walipozungumza na waandishi wa habari kuhusu tukio hilo, walidai mtuhumiwa alikuwa na matatizo ya akili. Walidai walipomhoji mtoto yuko wapi aliwajibu kwamba amempeleka kwa baba yake.
Leave a comment