KATIBU mpya wa itikadi na uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Amos Makalla, amesema chama hicho kitaendelea kumpa ushirikiano mtangulizi wake, Paul Makonda, katika majukumu yake mapya ya ukuu wa Mkoa wa Arusha. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Akizungumza katika hafla ya kuwapokea viongozi wa CCM walioteuliwa hivi karibuni, leo tarehe 5 Aprili 2024, jijini Dar es Salaam, Makalla amesema watampa ushirikiano kuenzi mchango wake mkubwa alioutoa kwa chama hicho, pindi alipokuwa katibu mwenezi.
“Leo nimepokea mikoba kutoka kwa mdogo wangu Makonda, amenikabidhi ofisi na kabrasha alilonikabidhi hili hapa limejaa majukumu yote na kazi alizoifanya, tunamshukuru kwa mchango wake alioufanya katika chama chetu na tunamtamkia kila la kheri katika nafasi yake ya ukuu wa mkoa,” amesema Makalla na kuongeza:
“Sisi tutaendelea kumpa ushirikiano wa chama katika kazi zake, lakini pia ameingia katika rekodi za makatibu wenezi ambao wamekifanyia kazi Chama Cha Mapinduzi, tunaheshimu mchango wake na mimi nitaanzia pale alipoishia kukisukuma, kukieneza chama.”
Kauli hiyo ya Makalla imekuja ikiwa siku moja tangu Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, wakati akimuapisha Makonda kuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha, kumsifu kiongozi huyo kwamba amefanya kazi nzuri CCM kwa kukichemsha na kuwaamsha viongozi wake waliolala.
Leave a comment