WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa, ameongoza mamia ya waombolezaji kuuga mwili wa aliyekuwa Mwenyekiti wa chama cha TLP, Agustino Mrema. Anaripoti Juliana Assenga, Dar es Salaam … (endelea).
Majaliwa ameongoza zoezi hilo leo tarehe 24 Agosti, 2022 mara baada ya kukamilika kwa ibada ya mazishi iliyoongozwa na Askofu Msaidizi Jimbo kuu la Dar es Salaam, Henry Mchamungu kwenye Parokia ya Mtakatifu Agustino iliyopo Salasala jijini Dar es Salaam.
Kabla ya kuaga mwili wa mwanasiasa huyo, Majaliwa alipata nafasi ya kutoa salamu za pole na kumuelezea jinsi anavyomfahamu mwanasiasa huyo mkongwe nchini.
Majaliwa alisema kuwa Mwanasiasa huyo ni mfano wa kuigwa kutokana na mambo aliyoyafanya kipindi akiwa Serikalini na hata upande wa Siasa.
“Tutamuenzi kutokana na mambo yake ambayo ameyafanya kipindi cha uhai wake katika upande wa serikali na kisiasa.
“Mrema amekuwa ni mfano wa kuigwa kwa serikali pamoja na siasa,” amesema.
Mrema aliyefariki Jumapili ya tarehe 21 Agosti, 2022, katika Hospital ya Taifa ya Muhimbili jijini Dar es Salaam anatarajiwa kuzikwa kesho Marangu – Kilimanjaro katika kijiji cha Kiraracha.
Leave a comment