SERIKALI imeamriwa kuwalipa kiasi cha Sh. 169.2 milioni, baadhi ya wakazi wa Loliondo mkoani Arusha, kama fidia ya kutaifisha mifugo yao kinyume cha sheria, kwa kigezo cha kuingia katika hifadhi ya Serengeti. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Amri hiyo imetolewa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma, jana tarehe 13 Februari 2024, katika kesi iliyofunguliwa na wafugaji wanne wakiongoza na Oloomu Kursas, kupinga mnada uliofanywa na Serikali kuuza mifugo yao kwa madai kuwa imekamatwa hifadhini kinyume cha sheria.
Taarifa ya uamuzi huo wa mahakama imetolewa leo tarehe 14 Februari 2024 na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), ambao ulitoa mawakili wa kuwatetea wafugaji hao.
“Tarehe 13 Februari 2024, Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma ilitoa uamuzi ulioeleza kuwa, mnada wa hadhara uliofanyika tarehe 1 Novemba 2023 kwa ajili ya ng’ombe 806, kondoo 420 na mbuzi 100 wa wafugaji kutoka Loliondo ulifanyika kinyume cha sheria. Mahakama iliamuru upande wa Jamhuri kurejesha kiasi cha shilingi za Tanzania 169, 264,200/= kwa Oloomu Kursas, Sinjore Maitika na Ndagusa Koros,” imesema taarifa hiyo.
Kesi hiyo ilifunguliwa baada ya Serikali mnamo tarehe 30 Oktoba 2023, kufungua kesi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Musoma, kuomba amri ya kutaifisha na kuuza kwa njia ya mnada mifugo, kwa madai kuwa haina mmiliki lakini pia imeingizwa hifadhini kinyume cha sheria.
Kufuatia kesi hiyo, tarehe 31 Oktoba 2023 mahakama hiyo ilitoa amri ya kutaifisha na kuuza mifugo iliyokamatwa. Mnada huo ulifanyika na kisha mifugo kuuzwa licha ya wamiliki wake kujitokeza na kuweka zuio mahakamani kutaka isiuzwe.
Wafugaji hao walikwenda Mahakama Kuu Kanda ya Musoma, kukata rufaa kupinga hatua hiyo ambapo iliamuru kesi ya awali isikilizwe upya. Baada ya kesi kusikilizwa wafugaji hao waliibwaga Serikali ambapo imetakiwa kulipa fidia.
Leave a comment