MAHAKAMA Kuu, Masijala ya Dar es Salaam imemzuia Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi kutoa fedha za ruzuku ya Chama cha Wananchi – CUF kwa Profesa Lipumba na wenzake, anaandika Pendo Omary.
Umauzi huo umetolewa leo mbele ya Jaji Dynsobela katika shauri Na. 28 la mwaka huu, ukilenga kusubiri kusikilizwa na kutolewa kwa maamuzi ya shauri Na. 21 la mwaka huu dhidi ya msajili na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (CAG) kutuhumiwa kutoa fedha za ruzuku Sh. 369 milioni za chama hicho kwa Prof. Lipumba na wenzake.
Shauri hilo dhidi msajili na CAG lilifunguliwa na jopo la mawakili wa CUF wanaoiwakilisha Bodi ya Wadhamini ya CUF, Daimu Halfani na Hashim Mziray.
Mawakili hao waliwasilisha maombi hayo mbele ya Mahakama Kuu kuiomba mahakama kutoa amri hiyo kwa kuwa fedha zilizotolewa awali 369 Milioni hazijulikani zimetumika vipi na hazikuwa katika mikono salama wala hakuna udhibiti wowote wa Chama cha CUF juu ya fedha hizo ikizingatiwa kuwa Lipumba alishavuliwa uanachama.
“Wakili Juma Nassor aliyewasilisha maombi hayo aliweka mkazo na kusisitiza kuwa kwa mazingira yaliyopo ni vyema na busara kwa fedha za umma zilizopaswa kutolewa kama ruzuku kwa CUF kwa sasa ziendelee kubaki serikalini,” amesema taarifa iliyotolewa leo na Kurugenzi ya Habari, Uenezi Na Mahusiano na Umma-CUF.
Aidha, mawakili hao wameiomba Mahakama Kuu amri hiyo pia ifungamane na kesi ya msingi Na. ya mwaka 2016 ya kuhoji maamuzi ya Msajili kumtambua Lipumba kwa nafasi ya uenyekiti iliyopo mbele ya Jaji Kihijo ambayo kwa sasa imekatiwa Rufaa ya kufanyiwa marejeo mbele ya Mahakama ya Rufaa-Tanzania.
Leave a comment