RAIS wa Tanzania, John Magufuli amesema, amefungua milango kwa sekta binafsi kuwekeza nchini huku akiahidi kuwashughulikia watendaji watakaokwamisha wawekezaji hao. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Kauli hiyo ameitoa leo leo Ijumaa tarehe 13 Novemba 2020, wakati akitoa hotuba ya kulifungua Bunge la 12, jijini Dodoma akieleza mwelekeo wa miaka mitano 2020 – 2025.
“Tutapitia upya kodi na tozo mbalimbali ikiwezekana kuzipunguza, tunakaribisha sekta binafsi kutoka ndani na nje ya nchi kuja kuwekeza kwa kuwa, tumebarikiwa na fursa nyingi ,” amesema Rais Magufuli.
Huku akishangiliwa na wabunge, Rais Magufuli amesema “tunahitaji kuwa na mabilionea wengi wa Kitanzania wakiwemo wabunge. Nataka Watanzania wote washiriki kikamilifu katika kujenga nchi yao.”
“Wakati wa kufanya mambo bila woga ni sasa. Tumechelewa sana. Katika miaka mitano ijayo tutafungua milango ya majadiliano na sekta binafsi ili kumaliza msuguano uliopo,” amesema akiwakaribisha kuwekeza kwenye viwanda vya mifugo
Aidha katika kusisitizia hilo, Rais Magufuli ameamua kuhamisha Kituo cha Taifa cha Uwekezaji (TIC) na Uwekezaji kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu na kukipeleka Ofisi ya Rais ili kutatua kwa haraka changamoto zinazoweza kujitokeza.
“Nataka mwekezaji mwenye fedha zake, akija apate kibali ndani ya siku 14. Nimeamua suala la Uwekezaji na Kituo cha Uwekezaji kuihamisha Ofisi ya Rais kutoka ofisi ya waziri mkuu ili hao wanaokwamisha nikapambane nao mimi mwenyewe ,” amesema
“Najua kulikuwa na ugumu au kucheleshwa kwa wawekezaji kupata vibali, ila kuanzia sasa nataka vibali vipatikane ndani ya siku 14” amesisitiza Rais Magufuli.
Amesema, kukua kwa sekta binafsi nchini kutaisaidia kuondoa changamoto mbalimbali hasa kwenye upande wa ajira sambamba na kuiingia nchi kipato.
Rais Magufuli amesema, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, sekta mbalimbali zilisaidia katika ustawi wa nchi ikiwepio sekta ya utalii ambayo iliajiri watu milioni nne.
Hotuba hiyo ya Rais Magufuli aliyoinza saa 3:57 asubuhi, aliihitimisha saa 5:22.
Baada ya kuhitimisha, Spika wa Bunge, Job Ndugai ameahirisha mkutano wa kwanza wa Bunge la 12 leo Ijumaa hadi tarehe 2 Februari 2021.
Leave a comment