KITUO cha Sheria na Haki za Binadamu nchini Tanzania (LHRC), kimeiomba Serikali iongeze viwango vya mishahara ya wafanyakazi wa sekta binafsi, ili vikidhi hali ya uchumi wa sasa. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Wito huo umetolewa leo Alhamisi, tarehe 29 Julai 2021 na Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Anna Henga, akizindua ripoti ya haki za binadamu na biashara nchini, ya mwaka 2020/21, mkoani Dar es Salaam.
“Tunaiomba Serikali ipitie na kuboresha au kubadili viwango vya mishahara ya wafanyakazi wa sekta binafsi, kwani waraka wa Serikali kuhusu viwango vya mishahara unaotumika ni wa 2013. Pamoja na kutumika unatakiwa kupitiwa kila baada ya miaka mitatu, kitu ambacho hakijafanyika,” amesema Henga.
Henga amesema kuwa, utafiti uliofanywa na LHRC kuhusu haki za binadamu na biashara, unaonesha wafanyakazi wengi wa sekta hiyo, hawatosheki na viwango vya mishahara wanavyopata.
Licha ya kupata viwango vidogo vya mishahara, Henga amesema utafiti huo uliofanyika katika mikoa 15 ya Tanzania Bara, unaonesha kwamba, wafanyakazi wengi wa sekta binafsi hawalipwi kwa wakati ujira wao.
“Haki zilziokiukwa zaidi kwa mwaka wa 2020/21, ni kutolipwa mshahara, kucheleweshewa malipo ya mshahara, usitishwaji ajira usio haki, punguzo la mshahara lisilo la haki,” amesema Henga.
Hivi hapa nchini kwetu tuna vyama vya wafanya kazi kweli? Ripoti kama hii walitakiwa waandike wao. Ni aibu kujiita vyama vya wafanya kazi. Ni udanganyifu na uzandiki. Afadhali vifutwe usajili badala ya kula fedha za wafanya kazi