MARA baada ya kutoka na ushindi wa mabao 2-1, kwenye mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Geita Gold Mine, kocha wa klabu ya Simba Pablo Franco martin ameonekana kutoridhishwa na kiwango cha timu yake, kiasi cha kuhofia hali itakavyokuwa kwenye mchezo wa marudiano dhidi ya Red Arrows nchini Zambia. Anaripoti Mwandishi Wetu….(endelea)
Mchezo huo wa duru la saba, ulipigwa jana majira ya saa 1 usiku kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam, na kuifanya Simba kuchukua alama tatu na kuendelea kusalia kwenye nafasi ya pili wakiwa na pointi 17, nyuma ya Yanga ambao ni vinara wakiwa na pointi 19.
Katika mchezo huo Simba ilionekana kuwa katika wakati mgumu mbele ya vijana wa Geita Gold ambao wananolewa na kocha Fred Felix Minziro, kutokana na ubora waliounesha licha ya kushindwa kutumia baadhi ya nafasi walizozipata.
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya mchezo huo kumalizika, kocha huyo alionekana kutoridhishwa na kiwango kilichooneshwa na Simba licha ya kucheza kwenye uwanja wao wa nyumbani mbele ya mashabiki wao.
“Leo (jana) sijaridhishwa na kiwango kilichjooneshwa na timu yangu, tulicheza mchezo mbaya hatukuonesha ubora wetu tuliopaswa kuwa nao katika mchezo huu, ukizingatia tunacheza nyumbani.” Alisema Pablo
Aidha kocha huyo alikwenda mbali zaidi, kiasi cha kuiongiwa na wasiwasi na kiwango kilichooneshwa na kikosi chake kuelekea mchezo wa marudiano ya kombe la Shirikisho barani Afrika dhidi ya Red Arrows.
“Kama tukicheza hivi tutakwenda kuwa na wakati mgumu nchini Zambia, nafikili itakuwa ni vigumu kwenda kupambania malengo yetu tuliyonayo.” Alisema kocha huyo
Katika mchezo wa kwanza uliopigwa Dar es Salaam, tarehe 28 Novemba 2021, Simba iliibuka na ushindi wa mabao 3-0, na mchezo wa marudiano utapigwa Jumapili Tarehe 5, Disemba 2021, Kitwe nchini Zambia.
Mara baada ya mchezo wa jana kikosi hiko kesho kitaanza safari ya kuelekea nchini Zambia kwa mchezo huo wa marudiano, ambapo kwenye mchezo huo Simba inahitaji sare au ushindi wa aina yoyote ili iweze kufuzu kwa hatua ya makundi ya michuano hiyo.
Leave a comment