Bodi ya Ligi imefanya marekebisho kwa michezo 12 ya Ligi Kuu Tanzania Bara, ukiwemo mchezo ulioahirishwa kati ya Kagera Sugar dhidi ya Simba ambao umepangwa kupigwa tarehe 26 Januari 2022. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Mchezo huo namba 69, hapo awali ulitakiwa kupigwa tarehe 18 Desemba, 2021 kwenye dimba la Kaitaba, lakini ilishindikana kufuatia wachezaji 16 kati ya wachezaji 22 wa Simba waliosafiri kwenda Bukoba kwenye mchezo huo kuonekana kuwa na dalili za mafua na kukohoa hali inayochangiwa na mabadiliko ya hali ya hewa.
Bodi ya Ligi waliahirisha mchezo huo kwa kutumia kanuni ya 34:1(1.3) ambayo inaeleza kuwa mchezo wowote wa Ligi Kuu unaweza kuahilishwa kwa sababu za dharura au yenye msingi itakayokubaliwa na Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini ‘TFF’
Katika taarifa yao waliyoitoa hii leo kwa waamndishi wa habari imeonesha kuwa mchezo huo utapigwa kwenye dimba Kaitaba tarehe 26 Januari, 2022 majira ya saa 12 jioni.
Ratiba kamili kwenye jedwari hapo chini
Mabadiliko hayo yamelenga kuepuka uwepo wa michezo ya viporo kutokana na ushiriki wa Simba kwenye Kombe la Shirikisho Afrika (CAFCC) huku michezo mitatu ikipangiwa tarehe baada ya kufahamika kwa hatma ya ushiriki wa klabu nne (Yanga, Simba, Azam na Namungo) katika michuano ya Kombe la Mapinduzi inayoendelea visiwani Zanzibar.
Ratiba ya awali ya Ligi Kuu ya NBC ilizingatia ushiriki wa klabu nne (Simba, Yanga, Azam na Biashara United) kwenye michuano ya CAF kwa kuzipatia nafasi ya kutosha kwa ajili ya maandalizi, safari na kucheza mechi za michuano hiyo nyumbani na ugenini.
Kuondolewa kwa klabu za Yanga, Azam na Biashara United kwenye michuano ya CAF, kumeilazimu Bodi ya Ligi kupitia upya ratiba ya Ligi na kufanya mabadiliko haya ili Ligi iendelee kuchezwa bila kuwa na mechi za viporo kwa timu yoyote ikiwemo Simba ambayo inaendelea na mashindano hayo.
Leave a comment