MAKAMU mpya Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana, amesema katika uongozi wake atahakikisha haki na demokrasia inaimarika ndani na nje ya chama hicho. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Kinana ametoa ahadi hiyo leo Ijumaa, tarehe 1 Aprili 2022, muda mfupi baada ya kuchaguliwa na wajumbe wa Mkutano Mkuu Maalumu wa CCM, uliofanyika jijini Dodoma, kushika nafasi hiyo iliyokuwa inashikiliwa na Mzee Phillip Mangula, aliyeng’atuka jana.
Mwanasiasa huyo amesema kazi yake ya kwanza, itakuwa ni kuiimarisha CCM ili kiwe chama imara kinachokubalika na kuheshimika kwa Watanzania, na kwamba ili azma hiyo ifanikiwe lazima demokrasia ndani ya chama hicho iwe imara.
“Ili demokrasia iwe imara, lazima tusimamie haki, haki ya kuchaguliwa na kuchagua bila upendeleo, mizengwe, rushwa na umaarufu,” amesema Kinana.
Kinana amesema, katika uongozi wake ataimarisha uhuru wa kutoa mawazo kwa wanachama wa CCM.
“Haki ya pili, ni haki ya kutoa mawazo, lazima wanachama wawe huru kutoa mawazo, hakuna mwenye haki miliki ya mawazo lazima tuwe tayari kusikiliza kila mwanachama na ndivyo tutakavyoweza kumsikiliza kila mwananchi,” amesema Kinana.
Aidha, Kinana amesema maamuzi ya WanaCCM katika kuchagua watu watakaogombea nafasi mbalimbali katika chaguzi, yataheshimiwa.
“Kwa hiyo lazima tuhimize demokrasia, tusimamie demokrasia, wanachama wakimchagua mtu kwani sisi ni nani wa kupinga? Inawezekana ikatokea sababu za kimaadili, lakini kimsingi wakimtaka mtu lazima tusimamie demokrasia, tulinde haki ya mtu kuchaguliwa na kuchagua. Tukiweza kuimarisha haki ndani, tutaimarisha nje ya CCM,” amesema Kinana.
Akizungumzia uteuzi wake, Kinana amesema alifanya mazungumzo na Rais Samia Suluhu Hassan, ambaye ni Mwenyekiti wa CCM, kwa saa mbili, ambapo alimueleza masuala anayohitaji amsaidie ndani ya chama na serikalini.
“Juzi jioni uliniita nikawa najiuliza naitiwa nini? Lakini nilimwambia Rais nimeitikia wito wako, niko tayari kukusikiliza, akaniambia nataka uwe makamu, nikamwambia sina hiari zaidi ya kusema nakubali,” amesema Kinana na kuongeza:
“Nilikwenda na kitabu na kalamu, nikamwambia niko tayari kukusikiliza, nikamsikiliza kwa masaa mawili, akanieleza mambo ya chama, Serikali, wananchi na matarajio yake anavyotaka nimsaidie. Napenda kukuhakikishia nitajitahidi kufikia matamanio yako.”
Na zile mali za chama zilizoporwa na wakubwa? Na ripoti yake utaitoa?