WANASIASA wakongwe nchini Tanzania, wamejadili sababu za kukwama kwa mchakato wa upatikanaji Katiba mpya na namna ya kuukwamua. Anaripoti Mwandishi Dodoma, Dodoma … (endelea).
Mchakato huo umejadiliwa leo Jumanne, tarehe 5 Aprili 2022, jijini Dodoma, katika kongamano la haki, amani na maridhiano, lililoandaliwa na Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD).
Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Tanzania Bara, Abdulrahman Kinana, amesema sababu za mchakato huo kukwama ni vyama vya siasa kutanguliza maslahi binafisi.
“Lakini moja lazima tukiri ambalo lilisaidia kukwamisha, kwa kila chama kung’ang’ania maslahi yake. Nadhani huo ndiyo ukweli lazima tuuseme, kulikuwa na mapendekezo yametolewa mambo yanekuja bungeni, yamejadiliwa watu wanakuja na mapendekezo kimoja kinasema hapana,” amesema Kinana.
Mwanasiasa huyo mkongwe nchini Tanzania amesema “wakati mwingine unaangalia zaidi mambo yanayohusiana namna gani utakuwa madarakani, kuliko namna gamin wananchi wanafaidika. Matokeo yake mnabaki kubishana, kwa sehemu kubwa mahusiano ya wananchi na mkwamo ni sehemu ndogo.”
Kinana amesema ili kutafuta suluhu ya mkwamo huo, vyama vya siasa vinapaswa kuzungumza ili kupata muafaka badala ya kubishana hadharani.
“Mimi nadhani ni muhimu tukatafuta nafasi sisi ambao ni vyama, tutakubaliana kukutana na kuzungumza. Tatizo kubwa tulilo nalo tunabishana nje hadharani, hatukutani. Hatujipi nafasi ya kuzungumza. Tukizungumza itapunguza mifarakano, tofauti zitapungua maelewano yatakuwa zaidi,”amesema Kinana.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo, Juma Duni Haji, amesema kukwama kwa mchakato wa upatikanaji katiba mpya, umesababishwa na wenye mamlaka kutolitaka jambo hilo.
Hata hivyo, Duni amempongeza Rais Samia Suluhu Hassan, kwa kuonesha nia kuhusu utekelezaji wa jambo hilo.
“Ninyi wenye madaraka kama hamtaki maridhiano hakuna maridhiano, kama mnataka maridhiano yawepo yatakuwepo, Lini tutarudi kwenye katiba tutatafuta matatizo yaliyokuwepo tuyamalize nchi inaweza kwenda. Lazima ustashi utoke kwa watu wenye power,” amesema Duni.
Duni amesema “mambo ya katiba kwa nini tulifeli? Nilikuwepo Dodoma, katiba ile haikumalizika kwa sababu watu wa CCM walikuja na katiba yao, wanataka lazima sote tuikubali na ikafika mahali wapinzani ili tusiwe sehemu ya katiba ya CCM, tukatoka nje ili inapopitishwa tusiwemo, hivyo katiba ile haikuwa na wapinzani.”
Leave a comment