CHANGAMOTO ya uhaba wa maji katika Jimbo la Musoma Vijijini, mkoani Mara, iko mbioni kuisha baada ya Serikali kupeleka miradi ya maji safi na salama katika vijiji vyake 68. Anaripoti Mwandishi Wetu.Mara … (endelea).
Suala hilo lililokuwa kilio kwa wananchi kwa miaka mingi, liko mbioni kuisha baada ya hivi karibuni Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Musoma (MUWASA), pamoja na mkandarasi kusaini mkataba wa utekelezaji mradi wa ujenzi wa miundombinu ya usambazaji maji katika vijiji sita vya kata za Tegeruka.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Mbunge wa Musoma Vijijini, Prof. Sospeter Muhongo, vijiji hivyo sita vilikuwa vimeachwa katika mradi wa maji kutoka bomba la Maji la Mugango-Kiabakari-Butiama.
Vijiji hivyo vinatarajiwa kuunganishwa katika bomba hilo baada ya mradi wake kukamilika ndani ya siku 180 (miezi mitatu), kutoka siku ya mkataba wa mradi uliposainiwa, tarehe 13 Aprili mwaka huu.
Leo tarehe 20 Aprili 2023, Ofisi ya Mbunge wa Musoma Vijijini, imeanisha hatua za utekelezaji wa miradi ya maji katika vijiji vyote jimboni humo, ambapo shughuli za usanifu wa ujenzi wa miradi zinakamilishwa katika vijiji 19, ambapo fedha zake zimetengwa katika bajeti ya mwaka wa fedha wa 2023/24, inayoanza Julai Mosi, 2023.
“Musoma Vijijini vijiji vyetu vyote 68 vina miradi ya maji safi na salama. Miradi hiyo ya maji iko kwenye hatua mbalimbali kama ifuatavyo,vijiji viwili vinatumia maji ya visima virefu. Vijiji 32 tayari vinatumia maji ya bomba kutoka Ziwa Victoria na usambazaji unaendelea ndani ya vijiji hivyo.
“Vijiji 15 tayari vimepewa fedha za miradi, na ujenzi wa miundombibu ya usambazi maji ya bomba kutoka Ziwa Victoria unaendelea,” imesema taarifa hiyo.
Kufuatia hatua hiyo, Prof. Muhongo ameiomba Serikali itoe kwa wakati fedha kiasi cha Sh. 2.5 bilioni, zilizotengwa katika bajeti ya mwaka ujao wa fedha, kwa ajili ya ukamilishaji miradi ya maji jimboni mwake, ili wananchi wapate maji safi na salama kwa uhakika.
“Shukrani nyingi na za kipekee ziende kwa Serikali yetu chini ya uongozi mzuri wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan. Nataka kuthibitisha kwamba, maombi yetu yako kwenye bajeti ya 2023/24 ya karibu bilioni 2.5 na tunaomba maombi yetu yafanyike,” amesema Prof. Muhongo.
Kwa upande wa wanavijiji wameishukuru Serikali kwa kupeleka miradi hiyo ambayo itawasaidia kuondokana na aza ya uhaba wa maji, huku baadhi yao wakieleza kwamba kwa sasa wanalazimika kuamka alfajiri kutafuta huduma hiyo mbali na maeneo wanayoishi.
Leave a comment