MKUU wa Mkoa wa Kilimanjaro, Stephen Kagaigai amesema mkoa huo umevunja rekodi kwa kupokea kiasi kikubwa cha fedha za maendeleo zilizotolewa na Serikali ya awamu ya sita katika kipindi cha miezi sita. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kilimanjaro … (endelea).
Kagaigai ametoa kauli hiyo leo tarehe 22 Januari, 2022 katika uwanja wa Chuo Kikuu cha Ushirika (MoCU) wakati wa uzinduzi wa Tamasha la utamaduni mkoa Kilimanjaro, ambalo Rais Samia alikuwa mgeni rasmi.
Akitoa salamu za mkoa huo kwa Rais ambaye pia ni Chifu Hangaya, Kagaigai amesema katika kipindi cha Julai hadi Desemba 2021, mkoa huo umepokea Sh bilioni 57.39 sawa na asilimia 40 ya bajeti yote ya maendeleo.
“Hiki ni kiwango kikubwa cha fedha za maendeleo kuwahi kupokelewa mkoani hapa katika nusu ya kwanza ya mwaka wa fedha wa Serikali. Kwa niaba ya wananchi wa Kilimanjaro tunakushukuru (Rais Samia) sana,”amesema.
Aidha, Kagaigai amesema mkoa huo ulipokea Sh bilioni 7.88 ambazo ni sehemu ya mkopo wa Sh trilioni 1.3 kutoka Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) kwa ajili ya ustawi na mapambano dhidi ya ugonjwa wa Uviko-19.
“Lakini mkoa ulipokea Sh bilioni 2.48 zinazotokana na tozo kwenye miamala ya simu, Sh bilioni 18 za ruzuku ya maendeleo kwa Serikali za mitaa na pia mkoa ulipata Sh bilioni 4.2 kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya za Kata.
“Pia mkoa huo ulipokea Sh milioni 418.1 ambazo ni fedha za mpango wa matokeo, Sh bilioni 22.44 kwa ajili ya matengenezo na ukarabati wa barabara na ukapokea Sh bilioni 1.9 kwa ajili ya miundombinu ya maji katika mkoa huo.
Amesema fedha zote zilizopokelewa zimeelekezwa kwenye ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya utoaji wa huduma katika sekta za Afya, Elimu, Maji, barabara na madaraja.
Pamoja na hayo amesema mkoa huo umefanikiwa kukamilisha ujenzi wa madarasa 276 ya shule za sekondari, ujenzi wa mabweni mawili ya wanafunzi wa elimu maalumu.
Ameongeza kuwa mkoa huo unaendelea na ujenzi wa shule tisa mpya za sekondari kwa kutumia fedha hizo za maendeleo.
Leave a comment