KATIBU Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo, Ado Shaibu, amesema vyama vya upinzani vilifanya makosa kuwapokea baadhi ya makada waliotoka katika chama tawala cha CCM, kisha kuwapa dhamana ya kugombea nafasi za uongozi katika chaguzi mbalimbali. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Ado ametoa kauli hiyo leo tarehe 2 Februari 2023, akihojiwa na Kituo cha Redio cha East Africa.
Mwanasiasa huyo amedai kuwa, baadhi ya wanachama hao baada ya muda hurejea CCM, ambapo amemtolea mfano Waziri Mkuu mstaafu Edward Lowassa, aliyehamia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na kupewa ridhaa ya kugombea urais katika Uchaguzi Mkuu wa 2015.
Pamoja na Waziri wa zamani wa Mambo ya Nje, Bernard Membe, aliyepokewa na chama chake kisha kumteua kugombea Urais wa Tanzania katika Uchaguzi Mkuu wa 2020, ambao wote katika nyakati tofauti walirejea CCM.
“Uzoefu unaonyesha wenzetu kutoka CCM kama wataondoka kwa tofauti zao baada ya muda kwa kauli yake yeye mwenyewe Mzee Membe, anasema wanakumbuka nyumbani maana yake anasema niliwa-miss sana nyumbani, sasa hilo ni funzo. Uchambuzi wangu ni kwamba Lowassa na Membe yalikuwa makosa ya vyama vya upinzani,” amesema Ado.
Katika hatua nyingine, Ado amevitaka vyama vya siasa vya upinzani kuandaa wanachama wake kushika nafasi nyeti za uongozi ikiwemo Urais, kama ACT-Wazalendo inavyofanya kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2025.
“Siasa ni mapambano ya hoja na ACT Wazalendo ndio Chama kinachokuwa kwa kasi nchini hivi sasa ukizungumzia vyama vitatu vikubwa vya siasa huwezi kuikosa ACT kwahiyo inapokuwa kwa kasi inatishia nafasi za watu na inazalisha minyukano,” amesema Ado.
Leave a comment