MJI mdogo wa Mirerani uliopo katika wilaya Simanjiro mkoani Manyara umeongeza bilione mpya wa madini ya Tanzanite baada ya mchimbaji mdogo Anselim Kavishe kupata vipande viwili vya madini hayo vyenye thamani ya Sh bilioni 2.2 bilioni.
Kavishe anakuwa bilionea wa pili wa madini hayo ya Tanzanite aliyetambuliwa na Serikali akitanguliwa na bilionea Saniniu Laizer ambaye mwaka 2020 alipata madini hayo yenye thamani ya Sh bilioni 7.8. Anaripoti Mwandishi Wetu, Manyara … (endelea).
Hayo yamebainishwa leo tarehe 27 Agosti, 2022 na Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Adolf Nduguru wakati akimtangaza Kavishe kuwa bilionea huyo mpya katika hafla ya ununuzi wa madini ya Tanzanite.
Amesema Kavishe amepata vipande viwili vya madini ya Tanzanite vyenye uzito wa kilogramu 3.74 na kilogramu 1.48.
Amesema kati ya madini hayo mawili yenye uzito wa kilogramu 1.48 ina thamani ya Sh milioni 713.8 na ya uzito wa kilogramu 3.74 yenye thamani ya Sh1.5 bilioni jumla ni Sh bilioni 2.245,” amesema Nduguru.
Aidha, Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole Sendeka (CCM) alimpongeza Kavishe kwa kufanikiwa kupata madini hayo.
“Hata mimi nisipokuwa bilionea, wananchi wangu wakiwa mabilionea ndiyo namimi nafarijika, tumezidi kuzalisha mabilionea wapya,” amesema Ole Sendeka.
Aidha, akizungumza baada ya kutangazwa katika hafla hiyo, Kavishe amesema anamshukuru Mungu kwa hatua hiyo ya kula matunda ya Tanzanite ambayo yeye pamoja na timu yake wameyatafuta kwa zaidi ya miaka 15.
Mbali na kumshukuru Rais Samia na viongozi wengine wa Serikali kwa ushirikiano wao, pia Kavishe amesema, “Sikutegemea kama kuna siku nitasimama mbele zenu kwa tukio kubwa kama hili katika maisha yangu, sina neno kubwa zaidi ya kuwashukuru,” amesema.
Leave a comment