JAMII imeaswa kuacha kujisaidia vichakani na badala yake imetakiwa kujenga na kutumia vyoo bora ikiwa ni pamoja na kunywa maji yaliyochemshwa na kunawa mikono kwa maji tiririka na sabuni ili kujiepusha na magonjwa ya kuhara. Anaripoti Ibrahim Yassin, Songwe …(endelea).
Hayo yamesemwa leo tarehe 11 Julai 2023 na Mratibu wa mazingira kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto (UNICEF), Gasten Gratien katika kikao cha tathmini ya utekelezaji wa mabadiliko ya tabia ya jamii kwenye masuala ya usafi, utunzaji wa mazingira na utumiaji wa vyoo bora mkoani Songwe.
Amesema katika kikao hicho wameshirikisha wadau mbalimbali wakiwemo viongozi wa serikali ngazi za vijijini, kata, wilaya hadi mkoa wakiwemo wazee wa mila na viongozi wa dini.
Amesema wananchi wa mkoa wa Songwe hasa vijijini walikuwa na uelewa mdogo katika hali ya usafi na utunzaji wa mazingira kwa muda mrefu na katika kuwaelimisha wametumia vyoo bora kutoka asilimia 0 mwaka 2021 hadi asilimia 46 mwaka 2023 sawa na asilimia 0-12.
Ameongeza kuwa wametoa elimu ya utekelezaji wa program za maji, afya na usafi wa mazingira katika vijiji wamebakiza asilimia 40 kukamilisha huku vijiji 150 viko katika hatua ya uhakiki wa ndani ambavyo vinategemea pia kufanyiwa uhakiki wa nje Julai.
Amesema matokeo yaliyopatikana katika semina hiyo ni kuongezeka kwa wahudumu wa vituo vya afya wenye elimu ya mabadiliko ya tabia ya jamii, ikiwemo kuongezeka kwa asilimia 53 ya walimu waliopata mafunzo ya afya, maji na usafi wa mazingira.
Ameeleza changamoto iliyopo kuwa ni baadhi ya viongozi wa siasa kupinga kampeni ya uhamasishaji kwa manufaa yao, mapungufu ya uelewa wa sheria za mazingira kwa baadhi ya watumishi ikiwemo kutofika vijijini kutoa elimu ya afya ya mazingira.
Mkuu wa mkoa wa Songwe, Dk, Fransis Michael, kupitia kikao hicho amesema kutokana na umuhimu wa mambo yaliyojadiliwa atawaagiza viongozi ngazi zote kutoa elimu kwa jamii kuhusu usafi wa mazingira, unawaji mikono na kutumia vyoo bora kwa kushirikiana na viongozi wa mila na dini.
Leave a comment