ZAIDI ya wakazi 13,051 wa vijiji vya Ntembo, Msia, Ikumbilo na Mlale kutoka wilaya ya Ileje mkoani Songwe wameiomba Serikali iharakishe ujenzi wa mradi wa maji Itembo ili kuondokana na kadhia yakutembea umbali wa kilomita nne kufuata maji. Anaripoti Ibrahim Yassin, Songwe…(endelea).
Wakizungumza jana tarehe 7 Julai 2023 mbele ya Katibu tawala mkoani Songwe, Happiness Seneda aliyetembelea mradi huo, wamesema kukamilika kwa mradi huo kutawaepusha na magonjwa ambukizi yanayotokana na uchafuzi kama vile kipindupindu.
Mmoja wa wakazi wa Ikumbilo, Anna Kayange amesema tatizo la uhaba wa maji limekuwa likikwamisha hata ukuaji wa sekta ya elimu kwa watoto huhangaika kuchota maji badala ya kwenda shule kusoma.
Akizungumzia hali hiyo, Kaimu Meneja wa Wakala wa Maji Safi na Usafi wa Mazingira (Ruwasa) wilayani Ileje, Mhandisi Brighton Pascal amesema mradi wa maji Ntembo ulioanza Machi 2023 chini ya mpango wa malipo kwa matokeo (P4R), unatarajiwa kukamilika Septemba 2023.
Amesema jumla ya Sh 455.7 milioni zimetumika kujenga mindombinu ikiwamo tenki lenye ujazo wa lita 500,000, vituo vya kuchotea maji na matenki madogo vya kupunguzia mgandamizo wa maji.
Ameongeza kuwa kazi nyingine iliyofanyika ni kulaza bomba, kuchimba na kufukia mtaro umbali wa kilomita 33 kazi iliyofanyika kwa gharama Sh 665.1 milioni na kufanya jumla ya gharama za mradi huo kuwa Sh 1.1 bilioni.
Amesema hadi sasa mradi upo asilimia 50 na kiasi cha Sh. 55 milioni kimetumika kwa ajili ya ununuzi wa bomba.
Amewaahidi wananchi kuwa wataongeza jitihada kuhakikisha mradi unakamilika haraka.
Katibu tawala mkoani Songwe, Happiness Seneda amesema kutokana na umuhimu wa mradi huo, ipo haja mamlaka husika kufanya kazi usiku na mchana kuhakikisha mradi unakamilika haraka.
Leave a comment