MAJINA 12 kati ya 17 ya waliofariki dunia katika ajali ya gari iliyotokea usiku wa kuamkia leo, Jumamosi tarehe 4 Februari, mkoani Tanga, yametajwa.
Majina hayo ni ya ndugu, familia na ukoo wa Athanas Cosmass Mrema, aliyefariki dunia jijini Dar es Salaam na basi lililobeba mwili wake kuelekea Rombo mkoani Kilimanjaro, kupata ajali jiji Tanga. Anaripoti Mwandishi Wetu, Tanga … (endelea).
Akizungumza na MwanaHalisi Online, ndugu wa marehemu Athanas Mrema, Novatus Tarimo amewataja watoto wa marehemu ambao wamefariki kwenye ajali hiyo kuwa ni Augustina Athanas Mrema na Nestory Athanas Mrema.
Amewataja ndugu wengine kuwa ni Lizybetha Linus Lamasey, Elizabeth Edward Mrema, Godwin Henry Mrema, Kenedy Joseph Mrema, Avelina Cosmas Mrema, Emiliana Colman Mrema, Rozina Andrea Lamosai, Suzana Matei Mrema, Julietha Edward Mrema na Ethan Peter.
Katika ajali hiyo miongoni mwa waliofariki, ni wanaume tisa na wanawake sita, wakiwamo watoto wawili mmoja wa kike na mmoja wa kiume.
Ajali hiyo ilitokea majira ya saa 4:30 usiku, eneo la Magila Gereza, katika barabara ya Segera – Buiko, lilihusisha gari aina ya Fuso na basi dogo aina ya Toyota Coaster, iliyokuwa ikitokea Dar es Salaam kuelekea Rombo, mkoani Kilimanjaro.
Basi hilo, lililokuwa na abiria 26, lilikuwa limebeba mwili wa Athanas Cosmass Mrema, aliyefariki dunia, katika Hospitali ya Bochi, iliyopo eneo la Kwa Msuguri Kata ya Saranga wilayani Ubungo, jijini Dar es Salaam.
Mkuu wa mkoa wa Tanga, Omary Mgumba, alidai kuwa chanzo cha ajali hiyo, ni uzembe wa dereva wa lori wa kuendesha gari lake kasi kwa kutaka kulipita gari la mbele bila ya kuchukua tahadhari, hivyo kugongana uso kwa uso na basi hilo.
Kwa mujibu wa Mgumba, miili ya marehemu imehifadhiwa katika hospitali ya wilaya ya Korogwe; majeruhi 10 kati ya 12 wamehamishiwa hospitali kuu ya mkoa wa Tanga (Bombo) na wawili wamebakishwa hospitali ya Korogwe kuendelea na matibabu.
Alisema, bado kuna miili ambayo haijatambulika.
Leave a comment