MBUNGE wa Musoma Vijijini, Profesa Sospeter Muhongo, kwa kushirikiana na wananchi wa kata ya Nyamrandirira, mkoani Mara, wamechangia fedha na vifaa mbalimbali kwa ajili ya ujenzi wa maabara tatu za masomo ya sayansi katika Shule ya Sekondari Seka. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mara … (endelea).
Michango hiyo imeanza kutolewa jana tarehe 3 Febrauri 2023, kupitia harambee iliyoongozwa na Prof. Muhongo, shuleni hapo.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini, wanavijiji wameamua ujenzi wa maabara hizo ukamilike ifikapo tarehe 30 Juni 2023.
Taarifa hiyo imechanganua ahadi na michango iliyotolewa, ambapo wananchi wameahidi kuchangia 15,000 kwa kila kaya, wakati Diwani wa Kata ya Nyamrandirira,Mwalimu Nyeoje akichangia Sh. 100,000, huku mbunge akihangia saruji mifuko 150, vitabu vya maktaba makasha saba na mahindi gunia nne kwa ajili ya chakula cha wanafunzi.
Katika hatua nyingine, wanakijiji na Prof. Muhongo wamepanga kununua kompyuta na mashine za utoaji nakala, ifikapo tarehe 30 Aprili 2023.
“Wanavijiji wa Kata ya Nyamrandirira na Viongozi wao mbalimbali wanatoa shukrani za kipekee kwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa mchango mkubwa, wa ujenzi wa Sekondari yao, unaotolewa wa Serikali anayoingoza ,” imesema taarifa hiyo.
Taarifa hiyo imesema kuwa, Shule ya Sekondari Seka yenye wanafunzi 344 kuanzia kidato cha kwanza hadi tatu na walimu tisa, inakabiliwa na changamoto ya upungufu wa maabara za masomo ya sayansi ya fizikia, kemia na bailojia, maktaba, jengo la utawala na choo chenye matundu saba. Shule hiyo ilianza rasmi tarehe 5 Julai 2021.
Leave a comment