MAELFU ya wanachama na wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), wanatarajia kushiriki maandamano ya amani yaliyoandaliwa na chama hicho, kudai katiba mpya na kupinga ugumu wa maisha. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha…(endelea).
Hayo yamebainishwa leo tarehe 26 Februari 2024 na Makamu Mwenyekiti wa Chadema Zanzibar, Salum Mwalim, akielezea maandalizi ya maandamano hayo yanayotarajiwa kufanyika kesho Jumanne, jijini Arusha, ambapo amesema yamefikia asilimia 97.
Mwalim amesema watu 1,000 jamii ya kimasai ni miongoni mwa washiriki wa maandamano hayo, ambao watayatumia kupaza sauti zao kupinga zoezi la Serikali kuwahamisha katika hifadhi ya Ngorongoro.
Mbali na wamasai, Mwalim amesema watu 1,800 kutoka mkoa wa Kilimanjaro na 2,300 kutoka Manyara, ni miongoni mwa waliojisairi kushiriki maandamano hayo ya hiari.
“Jamii ya wamasai zaidi ya 1,000 ambao watatoka eneo la Ngorongoro, Simanjiro na Tanga walikopelekwa ambao wamejiandikisha kushiriki maandamano hayo. Wengine ni jamii kubwa ya wafanyabiashara ndogo na wa kati Arusha,” amesema Mwalim na kuongeza:
“Mafuriko hayo yataonyesha haja na kiu ya matumaini ya watanzania wanayotaka. Yatabeba kielelezo halisi cha ugumu wa maisha, madai ya katiba mpya na miswada mitatu ambayo imepitishwa bungeni.”
Leave a comment