VIONGOZI wa dini kutoka madhehebu mbalimbali pamoja na wajasiriamali katika mkoani Kilimanjaro wamepatiwa bure mitungi ya gesi ya Oryx 1000 pamoja na majiko yake kwa lengo la kulihusisha kundi hilo katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia na kuachana na matumizi ya kuni na mkaa. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Mitungi hiyo ya gesi ya Oryx na majiko yake imetolewa na Kampuni ya Oryx Gas kwa kushirikiana na Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Kilimanjaro, Shally Raymond ikiwa ni sehemu ya mipango na mikakati ya kuunga mkono jitihada za Rais Samia Suluhu Hassan za kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa Watanzania.
Akizungumza wakati wa hafla ya kukagwa mitungi hiyo kwa viongozi wa dini na wajasiriamali wa mkoa huo, Naibu Waziri wa Nishati, Judith Kapinga amewaomba viongozi wa dini kutumia nafasi zao kusaidia jamii kutambua umuhimu wa kutunza mazingira kwa kuachana kutumia kuni na mkaa.
“Unaweza kutafakari na kujiuliza kwanini Mbunge Shally Raymond na Kampuni ya Oryx wameamua kuwaita viongozi wa dini kuhamasisha utunzaji mazingira? Ni kwasababu viongozi wa dini ni watu wa thamani sana, unajua sisi binadamu watu ambao tunawathamini na kuwasikiliza ni viongozi wetu wa dini na mimi kwa utashi wangu mdogo naamini tunawasikiliza viongozi wa dini kwasababu kazi ya kueneza neno la Mungu hakuna anayelipwa.
“Kwa maana hiyo ndio maana mama Shally pamoja na makundi mengine yote aliamua kuleta viongozi wa dini kwakuwa sisi tunawaheshimu, tuna matumaini makubwa na viongozi wa dini. Tunaamini viongozi wa dini ndio ambao wanaweza kutusaidia kuwaelimisha na kuwaambia wananchi kuhusu kutunza mazingira,” amesema Kapinga
Amesisitiza kwa watu wengine ambao hawana sura ya ki- Mungu ni ngumu kuaminika ndio maana wanasikilizwa zaidi na waumini wao.
Ameongeza kuwa uharibifu wa mazingira unatokana na ukataji miti umesababisha hata mikoa iliyokuwa na mvua nyingi kama mikoa ya nyanda za juu kusini ambazo zilitakiwa mvua kuanza Novemba zinaanza mwishoni mwa Desemba.
“Kwahiyo tunaamini viongozi wa dini mpo katika nafasi ya kutusaidia kuendelea kukumbusha jamii kwamba dunia hii ambayo tumepewa zawadi na Mwenyezi Mungu ni haki ya kila mmoja kuilinda leo, tuna watoto na wajukuu na tutakuwa na vitukuu pia, sasa kama rasilimali zote tulizonazo tutazichezea leo hawa wajukuu na vitukuu wataishi katika mazingira gani?”alihoji Naibu waziri huyo.
Amesema ni vema kuendelea kulinda mazingira yetu kwa ajili ya wengine na kuwahusisha viongozi wa dini ni muhimu kwasababu ni kundi ambalo linasikilizwa na hivyo amewaomba kusaidia katika ajenda hiyo ya nishati safi ya kupikia
Pia amesema kuwa katika kampeni hiyo ya kuhamasisha matumizi ya nishati ya kupikia wamekuwa wakihusisha zaidi wanawake kwasababu wanawake ndio wanaokaa jikoni kupika kuandaa chakula.
“Tunawashukuru Oryx kwa kutupatia majiko ya gesi lakini njia za nishati safi ya kupikia ni ile tu kasumba kwamba hii ni gharama lakini ndugu zangu kibaba cha mkaa wa Sh.2000 jioni hakifiki. Ni gharama nafuu kutumia nishati safi kuliko kutumia kuni na mkaa katika kuandaa chakula,” amesema.
Aidha, amesema pamoja na uwepo wa changamoto zinazotokana uharibifu wa mazingira bado kuna fursa kwa jamii kujirekebisha kwa kulinda mazingira.
Akizungumzia kampeni ya nishati safi ya kupikia, Naibu Waziri Kapinga amesema mwaka jana mwishoni kulikuwa kuna mkutano wa dunia wa mazingira na katika mkutano huo Rais Samia Suluhu Hassan alienda na ajenda mahususi ya kumkomboa mwanamke wa Afrika sio mwanamke wa Tanzania peke yake.
“Kumkomboa vipi? Kuweka mikakati ya kuhakikisha wanawake wote wa Afrika wanatumia nishati safi ya kupikia na katika mkutano ule ulihusisha wakuu wa nchii. Rais Samia kutokana na umahiri wake na uwezo wake aliweza kukusanya viongozi na kuzindua program maalum kusaidia wanawake wa Afrika kwenye kutumia nishati safi ya kupikia.
Kwa upande wake Meneja Mauzo wa Kampuni ya Oryx Gas Tanzania, Shaban Fundi aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa kampuni hiyo, Benoite Araman ametumia nafasi hiyo kueleza kuwa kwa muda mrefu sasa wamekuwa wanajivunia kuwezesha makundi mbalimbali yakiwemo wanawake, watoto na wajasiriamali kupata nishati safi ya kupikia.
“Kufanya hivyo tunaamini tunaikomboa jamiina taifa kwa ujumla wake kwani kupika kwa gesi ya Oryx kuna maanisha kuboresha afya za kinamama kwa kueuka kuvuta moshi mbaya wa kuni na mkaa. Pia tunaweza watoto kupata muda wa kwenda shule badala ya kutumwa kutafuta kuni,”amesema Fundi.
Amesisiza kampuni hiyo kwa kutambua nafasi ya viongozi wa dini imeona ni vema sasa ikatoa mitungi ya gesi ya Oryx na majiko yake kwa kundi hilo sambamba na kuelezea kwa kina umuhimu wa kutunza mazingira na wanaamini kuwa viongozi wa dini wana nafasi kubwa ya kusema na kusikilizwa, hivyo watakapokuwa mabalozi wa kuzungumzia nishati safi ya kupikia jamii itabadilika na hivyo kuokoa mazingira.
Aidha amekumbusha kuwa mwaka 2021 Rais Samia alianzisha kampeni ya nishati safi ya kupikia na alitoa maono yake ya kwamba ifikapo mwaka 2032 asilimia 80 ya wananchi itumie nishati safi, hivyo kuanzia hapo Oryx iliongeza nguvu na hadi sasa ya mitungi 19000 bure yenye thamani isiyopungua Sh. 1.5 bilioni.
Leave a comment