MWANASIASA mkongwe nchini Tanzania, Dk. Wilbroad Slaa, ambaye alikuwa kinara kumtuhumu kwa ufisadi aliyekuwa Waziri Mkuu mstaafu, Edward Lowassa, amesema hana doa naye baada ya kiongozi huyo kufariki dunia na kwamba anaiombea roho yake ipumzike kwa amani mbinguni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mwanza … (endelea).
Dk. Slaa ametoa kauli hiyo jana Jumatano, jijini Mwanza, akizungumzia kifo cha Hayati Lowassa, kilichotokea Jumamosi iliyopita kwenye Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), alikokuwa anapatiwa matibabu.
“Mimi niliwahi kutamka kwamba Lowassa ni fisadi Mwembeyanga, wala sikuficha lakini naomba niseme mimi pia ni Padri wengi mnajua lengo la Padri ni kuhakikisha binadamu wakimaliza maisha duniani unamuingiza mbinguni hata kama alikuwa mkosefu. Kwa hiyo mimi baada ya Lowassa kufariki yale yalishaisha natafuta namna ya kuingiza roho yake mbinguni hivyo sina doa tena hata kama nilisema ni fisadi,” alisema Dk. Slaa na kuongeza:
“Mimi leo hii ni nani kumhukumu Lowassa katika dakika yake ya mwisho? Yale ya duniani yamekwisha sisemi kwa sababu sina rekodi, rekodi zangu zote zipo mpaka leo, yale niliyoyasema ya ufisadi kwa sababu nilienda mpaka sekretarieti ya maadili ya viongozi nilikuwa na rekodi zeote.”
Lowassa enzi za uhai wake, alikabiliwa na tuhuma mbalimbali za ufisadi ambazo zilipelekea ajiuzulu uwaziri mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania 2008. Hata hivyo, mara kwa mara amekuwa akikanusha tuhuma hizo zinazotajwa kusukumwa na vita ya madaraka katika uongozi wa kisiasa.
Leave a comment