VIONGOZI wa kimila wa jamii ya Wamasai (Malaigwanan), wameomba aliyekuwa Waziri Mkuu mstaafu, Hayati Edward Lowassa, azikwe kimila kwa kuwa enzi za uhai wake alikuwa na hadhi kubwa ya kimila, baada ya kusimikwa kuwa mwenyekiti wa Malaigwanan wa Tanzania na Kenya. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha … (endelea).
Ombo hilo limetolewa jana Jumatano na Katibu Mkuu wa Malaigwanan Tanzania, Amani Lukumay, siku chache kabla ya mwili wa Lowassa kuzikwa nyumbani kwao Monduli mkoani Arusha, Jumamosi ya tarehe 17 Februari 2024.
“Lowassa tulidhani alishapanda kwenye ngazi ya juu atakuwa mtu mwenye uwezo wa kutuunganisha, tulimpa nafasi kuwa mwenyekiti wa Malaigwanani Tanzania na Kenya, kwa ahiyo alikuwa na hadhi kubwa sana kimila. Kwa mtu kama huyu akifariki kimila moja kwa moja na viongozi wa kimila wanakutana na familia kutaka kuleta maelewano wakati wa maziko,” alisema Lukumay.
Alisema “tunajua alikuwa na imani yake ya Kilutheri (Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania-KKKT), lakini pia alifanya kazi kwenye masuala ya mila, tulitaka ingelikuwa vizuri watu wa siasa wakamaliza kazi yao, lakini pia waombaji, maaskofu wa kilutheri wakamaliza kumuombea ili shughuli itakayobakia (mazishi) ifanyike kimila sababu hata mila imetoka kwa Mungu na hata yeye alikuwa akiamini katika haya.”
Kiongozi huyo wa Wamasai, alisema kwa mujibu wa mila zao, mtu mwenye hadhi ya Lowassa akifariki dunia viongozi wao huongoza zoezi la kuchinja kondoo aliyenona kisha mafuta yake huchukuliwa kwa ajili ya kuwapaka wajukuu pamoja na mwili wa marehemu kama ishara ya kumuaga kwa mara ya mwisho.
Kisha, hukalisha mwili wake katika kigoda ndani ya kaburi kwa ajili ya mazishi.
“Kwa hiyo tusimnyime lile ambalo lilikuwa tamanio lake sababu haliaribu lolote , mi naamini Mungu alikubali. Tungetamani taratibu za kumuaga kimila zingefanyika, mtu mkubwa akifa anachinjiwa kondoo safi mwema wakubwa watampaka mafuta yake kama njia kwamba kwa kheri kalale salama halafu ataingizwa ataketishwa kwenye kiti kizuri pale kaburini,” alisema.
Leave a comment