RAIS wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), Dk. Edward Hoseah, ameshauri wanasiasa kuvumiliana pindi wanapokinzana katika hoja na sera, kwa kuwa Tanzania ina mfumo wa vyama vingi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Dk. Hoseah ametoa wito huo jana tarehe 28 Julai 2021, akihojiwa na televisheni ya mtandaoni ya Wakili, inayomilikiwa na TLS, kuhusu masuala mbalimbali yanayoendelea nchini.
“Ninachosisitiza ni kwamba, nchi yetu ni ya vyama vingi, nashauri tuwe na uvumilivu. Sioni kwa nini uone vibaya kusikia mawazo ya wengine hasa ya wanasiasa, nashauri tukubali kusikia mawazo mbadala, si kosa wala dhambi. Sheria zinasema vyama vingi ni ruhsa,” alisema Dk. Hoseah.
Rais huyo wa TLS, alishauri wanasiasa wajifunze kuheshimu maoni na mawazo yanayotoka kwa wapinzani wao, yanayotolewa kwa kufuata sheria za nchi.
“Tusibane mtu kutoa mawazo yake na fikra zake, as long as (maadam) hatukani, hamfanyii mwingine baya na havunji sheria. Hiyo ndiyo mipaka. Lakini mtu kutoa mawazo yake tofauti na chama tawala si kosa na chama tawala kijifunze kwa wengine, kama mawazo yake bora wayatumie katika sera zao,” alisema Dk. Hoseah.
Dk. Hosea alishauri vyama vya siasa viheshimu dhamira ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, ya Tanzania kuwa na mfumo wa vyama vingi.
Alisema, Mwalimu Nyerere alipohojiwa na iliyokuwa Tume ya Jaji Francis Nyalali, iliyoundwa 1991 na Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi, kuhusu mabadiliko ya mfumo wa vyama vya siasa, alishauri nchi iingie kwenye mfumo wa vyama vingi.
“Wakati wa Tume ya Jaji Nyalali, tulimhoji Mwalimu Nyerere swali lililouliza hapa tulipofika tuendelee kuwa na chama kimoja au vingi , alisema mtafanya makosa kama mtaamini mfumo wa chama kimoja, akashauri wachache wanaotaka vyama vingi wapewe mfumo huo,” alisema Dk. Hoseah.
Tume hiyo iliundwa kwa ajili ya kukusanya maoni ya wananchi, juu ya kuendelea na mfumo wa chama kimoja au kuwa na mfumo wa vyama vingi.
Baada ya mapendekezo ya tume hiyo, 1992 Serikali ya Tanzania ilifanya marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Siasa, Sheria ya Taifa ya Uchaguzi na Sheria ya Uchaguzi ya Serikali za Mitaa, yaliyowezesha mfumo wa vyama vingi vya siasa kutumika nchini.
Leave a comment