SERIKALI ya Tanzania, inatarajia kuingiza aina tano za chanjo ya Ugonjwa wa Korona (UVIKO-19), ili kukabiliana na maambukizi ya ugonjwa huo kwa wananchi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumatano, tarehe 28 Julai 2021 na Waziri wa Afya, Dk. Dorothy Gwajima, akizungumza katika uzinduzi wa chanjo ya UVIKO-19, Ikulu jijini Dar es Salaam.
Waziri huyo wa afya ametaja chanjo hizo kuwa, ni Moderna, Pfizer-BioNtech, Johnson &Johnson, Sinopharm na Sinovac.
Dk. Gwajima amesema, Serikali imeamua kuleta aina nyingi za chanjo, ili kila mwananchi apatiwe chanjo inayoendana na afya yake.
“Hakuna dawa isiyokuwa na mashara lakini kuna faida zake, ndiyo dawa ziko hivyo na jinsi ya ku-manage na daktari kukuona wewe nisikupe hii, nikupe mbadala,” amesema Dk. Gwajima na kuongeza:
“Ndiyo maana chanjo zitakuja nyingi, aina tano ili wananchi wafanye maamuzi, wazisome tuone huyu ana-fit hapa.”
Tarehe 24 Julai 2021, Serikali ya Tanzania ilipokea dozi 1,058,400 za chanjo ya Korona , kutoka katika Serikali ya Marekani, kupitia mpango wake wa Covax. Unaolenga kusaidia nchi zinazoendelea katika kukabiliana na janga hilo. Chanjo hizo ni aina ya Johnson & Johnson.
Leo Rais Samia Suluhu Hassan, anatarajiwa kuchanjwa chanjo hiyo, Ikulu jijini Dar es Salaam.
Leave a comment