MKUU wa Wilaya ya Dodoma, Alhaji Jabir Shekimweri ameeleza kukerwa uchafu uliokithiri katika kata ya Madukani Jijini Dodoma licha ya kuwa inaongozwa na Diwani wa kata hiyo Prof.Davis Mwanfupe (CCM) ambaye pia ni Meya wa Jiji la Dodoma. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Jabir ametoa kauli hiyo baada ya kumaliza ukaguzi wa mitaro ya maji taka katika barabara ya saba na ya nane na kueleza kuwa uchafu unaotupwa katika mitaro hiyo hauwezi kuvumilika.
Amesema kuwa katika ziara hiyo ya usafi ikiwa ni kampeni maalumu ya usafi katika jiji la Dodoma.
Aidha, Jabir ameeleza kusikitishwa kuona wakati wa usafi wenyeji ambao ni wafanyabiashara wamekaa ndani wakati wanaofanya usafi ni wageni.
Akizungumzia baadhi ya wananchi 14 ambao wamekamatwa kwa kuhusika na makosa mbalimbali ya uchafuzi wa mazingira kwa makusudi, Jabir amesema watu hao wanatakiwa kupigwa faini bila kusamehewa ili iwe fundisho kwa watu wengine ambao wamekuwa wakidharau sheria ya mazingira.
Katika hatua nyingine kiongozi huyo amesema kuwa suala la usafi halitakiwi kutungiwa sheria kubwa au kuhimizana mara kwa mara bali inatakiwa kuwa tabia ya kila mtu kuanzia nyumbani kama vile mtu anavyojiongoza kuoga au kufua nguo zake.
Leave a comment