MAMLAKA ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) nchini Tanzania, inatekeleza mradi wa majitaka Uhuru katika Wilaya ya Ilala jijini humo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Mradi huo unagharimu kiasi cha shilingi milioni 539, inayotokana na fedha za ndani za mamlaka hiyo, unakwenda kujibu kero ya majitaka kwa wakazi wa Ilala.
Msimamizi wa mradi huu, Mhandisi Justine Kyando akizungumza mwishoni mwa wiki hii, amesema utahusisha uchimbaji wa mitaro na ulazaji wa bomba zenye ukubwa wa inch nane umbali wa Kilomita 2 na mita 442.
Pia amesema, kutakuwa na ujenzi wa chemba za majitaka 48 katika maeneo mbalimbali.
Naye Mstahiki Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Mheshimiwa Omary Kumbilamoto amesema, Serikali itaendelea kutekeleza miradi kama hiyo sehemu mbalimbali za jiji hilo ili kufanya mazingira kuwa safi na salama.
“Nia ya serikali ni kuona wananchi wake wanakuwa katika mazingira masafi na kuepukana na matatizo ya kiafya ambayo yanasababishwa na uchafuzi wa mazingira kwa kutiririsha majitaka hovyo mitaani,” amesema Kumbilamoto.
Hivi karibuni, Mbunge wa Ilala (CCM), Mussa Zungu aliiomba DAWASA kuongeza mikakati ya tatizo la majitaka katika jimbo lake kwani imekuwa kero.
Zungu ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bunge alisema, maeneo mengi ya Ilala yanapata majisafi na salama lakini shughuli ipo kwa majitaka jambo ambalo aliitaka DAWASA inayohudumia mikoa ya Pwani na Dar es Salaam kueleza nguvu eneo hilo.
Miongoni mwa wanufaika wa mradi huo, Michael Lema ameishukuru serikali kwa kupeleka mradi huo katika mtaa wake kwani utakwenda kupunguza changamoto za utiririshaji majitaka katika eneo hilo.
“Tumefarijika kwa kuanza utekelezwaji wa mradi wa uhuru katika mtaa wetu kwani utaenda kupunguza kero kubwa ya utiririshaji majitaka katika maeneo mengi yatakayo tekelezwa mradi, hivyo kupunguza magonjwa ya mlipuko yasababishwayo na utiririshaji majitaka,” amesema Lema
Mradi wa majitaja Uhuru ulianza kutekelezwa Mei mwaka huu na unatazamiwa kukamilika ifikapo Septemba mwaka huu huku utekelezaji wake ukiwa umefikia asilimia 92 katika uchimbaji, ulazaji wa bomba, pamoja na ufukiaji.
Mradi huo wa majitaka uhuru utanufaisha zaidi ya kaya 350 katika mitaa ya Uhuru road, Utete, Kigoma, Mwanza, Arusha, Tukuyu, Moshi, Tabora, Morogoro pamoja na Tunduru yote iliyopo Ilala jijini Dar es Salaam.
Leave a comment