CHAMA cha Wauguzi Tanzania (TANNA) kimetoa taarifa ya uchunguzi wa tukio la watumishi wa kada ya Afya wa Zahanati ya Ishihimulwa wilaya ya Uyui mkoani Tabora waliokuwa wanazozana kuhusu kutumia vipimo vya malaria RDT ambavyo mmoja wao alidai vimeisha muda wake wa matumizi na kubainisha kuwa kulikuwa na mgogoro binafsi baina yao. Anaripoti Mwandishi Wetu, Tabora … (endelea).
Taarifa ya uchunguzi huo imetolewa leo Alhamisi tarehe 12 Januari 2023 na Ofisi ya Uenezi na Habari ya chama hicho ikiwa ni siku chache tangu kutokea kwa tukio hilo.
Itakumbukwa kuwa hivi karibuni katika mitandao ya kijamii ilisambaa video ikimwonesha mtaalamu wa maabara James Chuchu akizozana na muuguzi Rose Shirima kuhusu matumizi ya vipimo vya malaria ambavyo vilidaiwa kuwa vimeisha muda wake.
Katika video hiyo muuguzi alisisitiza mtaalamu huyo atumie vipimo hivyo kwa wajawazito huku akimtupia maneno ya kejeli kuwa ana kiherehere cha kutaka kuwa mfanyakazi bora.
Hata hivyo taarifa ya TANNA imebainisha kuwa mtaalamu wa maabara alimtusi muuguzi kabla ya kuanza kurekodi kitendo ambacho kilimfanya muuguzi atoe majibu yasiyo na staha.
Chama kimebaini uwepo wa mgogoro wa muda mrefu baina ya hao watumishai na hata hivyo kabla ya kuanza kurekodi video kulikuwa na lugha ya matuzi kutoka kwa mteknolojia wa maabara kwenda kwa muuguzi hali iliyomfanya muuguzi kufadhaika na kujikuta akimjibu kwa lugha isiyo na staha,” imeeleza taarifa hiyo.
Katika hatua nyingine chama hicho kimewatoa hofu wananchi wanaopata huduma kwenye Zahanati hiyo kuwa hakuna vitendanishi vyovyote vilivyoisha muda wake ambavyo vilikuwa vinatumika katika kituo hicho.
Chama hicho kimewakumbusha watumishi wa Afya kujenga utamaduni wa kuwa na vikao vya ndani na kuanzisha kamati za maadili kuanzia ngazi ya vituo ili kusaidia kutatua matatizo ya kitaaluma kwa wakati.
Leave a comment