SERIKALI imesema kumeguka kwa sehemu ya Mlima Hanang ambao ilikuwa una miamba dhoofu iliyonyonya maji ndio chanzo cha maporomoko yaliyoleta maafa katika eneo hilo la Hanang mkoani Manyara. Anaripoti Faki Sosi …(endelea).
Maporomoko hayo ya matope yamesababisha vifo vya watu 65 na majeruhi zaidi ya 100 huku mamia ya wanachi wilayani Hanang wakipoteza mifugo, mashamba na makazi yao kwa ujumla.
Akitoa taarifa kuhusu chanzo cha maporomoko hayo Msemaji wa Serikali, Mobhare Matinyi amesema Serikali ilituma wataalam wa madini ambao wamefanya uchunguzi tangu tukio lilipotokea.
Amesema wataalaam hao walifanya ukaguzi kwa njia ya miguu pamoja na Helkopta za jeshi la Wananchi la Tanzania na kufanikisha zoezi hilo.
“Taarifa fupi ya chanzo inasema kwamba imetokana na kumeguka sehemu ya Mlima Hanang ambayo ilikuwa ina miamba dhoofu iliyonyonya maji na hatimaye kusababisha mporomoko na hivyo kutengeneza tope.”
“Sehemu iliyonyonya maji ilizua mgandamizo na sehemu ya Mlima ikashindwa kuhimili mgandamizo na hivyo kusababisha kumeguka kwa sehemu hiyo na kutengeneza tope ambalo ndio lilianza kuporomoka kufuata mkondo wa mto Jorodom uliozoa mawe na miti na kushambulia makazi ya binadamu yaliyokuwa pembezoni mwa mto huo,” amesema Matinyi.
Amesema Mlima Hanang uliumbwa kwa miamba laini yenye chembechembe za mchanga wa Volcano.
Ameongeza kuwa serikali ilifuatilia taarifa za matetemeko kuanzia mwezi Septemba mwaka huu hadi siku ya tukio na kubaini kuwa hapakuwa na tetemeko lolote na wala hakukuwa na mlipuko wa Volcano ikimaanisha kwamba tatizo la miamba laini kunyonya maji ndiko kulikosababisha maporomoko hayo.
Amesema licha ya wataalam kufanya uchunguzi huo, bado wanaendelea na uchunguzi zaidi.
Serikali imesema itawaonda wananchi ambao hawajaathirika la maporomoko hayo ya matope pamoja na wale walioathirika na janga hilo.
“Serikali itawaondoa wananchi ambao hawajaathirika, waliopo pembeni mwa eneo ambalo matope, mawe na maji yalipokuwa yakupita ili kuwaepusha na lolote linaloweza kutokea kutokana na mvua za Elnino kuendelea hapa nchini”
Hata hivyo, Serikali imebainisha kuwa tayari miili 60 imeshatambuliwa tayari.
Kati ya watu 65 waliopoteza maisha, maiti 60 zimeshachukuliwa kwa taratibu za mazishi, tano hazijatambuliwa hivyo Mkemia Mkuu wa Serikali atafanya utaratibu wa vipimo vya DNA ili kutambua ndugu zao ni akina nani.
“Serikali itaendelea kutoa matibabu bure kwa waathirika wate, kutoa chakula kwa manusura wengine ambao wamepoteza makazi na majeruhi wanaotoka hospitali,” amesema.
Amesema Serikali inaendelea na zoezi la uondoaji wa tope katika mji wa Kateshi ili kurejesha shughuli za kiuchumi.
“Bado juhudi za kufukua mali na nyumba zinaendelea na kutafuta iwapo kuna miili yoyote”
Amesena kuwa Serikali imerejesha huduma ya maji na umeme kwenye mji wa Kateshi sambamba na kudhibiti usalama kwa kutumia jeshi la Polisi.
Leave a comment