CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimewataka wanachama wa vyama vya siasa hususan Chama Cha Mapinduzi (CCM), kushiriki maandamano waliyoyaandaa kupinga ugumu wa maisha na kudai katiba mpya, kwa kuwa athari zake hazibagui mtu kulingana na itikadi zake. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mwanza…(endelea).
Wito huo umetolewa leo tarehe 14 Februari 2024 na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Bara, Benson Kigaila, akizungumzia maandalizi ya awamu ya pili ya maandamano hayo ya amani yanayotarajiwa kufanyika kesho Alhamisi, jijini Mwanza.
“Chama chetu tumeamua kwa niaba ya Watanzania, ni kazi ya kufa na kupona kwa sababu ni lazima serikali ya watu isikilize watu. Hatuwezi kuwa na serikali ambazo hazisikilizi watu, Serikali kwenye demokrasia hafifu kama yetu zinawekwa na watu lazima zisikilize watu hivyo tunataka serikali hii iwasikilize watanzania,” amesema Kigaila.
Kigaila amesema “ugumu wa maisha hauchagui kabila wala itikadi za kisiasa wote tunacharazwa viboko vilevile sababuy masoko yetu yaleyale. CCM huwa wanajidanganya wakati wa kampeni wanasema wataisoma namba wanadhani tutaisoma sisi lakini tukimaliza uchaguzi na wenyewe wanashuka tunarudi nyuma tunaisoma namba CCm iko mbele kwa mbele.”
Kigaila amewataka viongozi wa vyama vya siasa kushiriki maandamano hayo ili kudai katiba mpya na kupinga miswada ya marekebisho ya sheria za uchaguzi ambayo imepitishwa bungeni hivi karibuni kwa ajili ya kuwa sheria baada ya kusainiwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.
“Maandamano haya tumeamua tuandae kwa niaba ya watanzania wote wanaoteseka, yanalenga kila mtanzania mpenda haki na anayeumia. Tunawaalika taasisi zote bila kujali vyama vyao waje tuungane. Vyama vya siasa vyote waje tuungane sababu ni taasisi zilizosajiliwa kuusemea umma ukiwa kwenye shida,” amesema Kigaila.
Awamu ya kwanza ya maandamano hayo ilifanyika Januari mwaka huu jijini Dar es Salaam, ambapo msafara wake uliishia katika ofisi za Umoja wa Taifa (UN)nchini, zilizoko jijini humo, kisha kuwasilisha mapendekezo yao kwa ajili ya taasisi hiyo ya kimataifa kutoa wito kwa Serikali iyafanyie kazi.
Leave a comment