CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema awamu ya pili ya maandamano ya amani yanayotarajiwa kufanyika tarehe 22 hadi 30 Aprili 2024, yatafanyika kwenye kanda nne. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari Leo Alhamisi, jijini Dar es Salaam, Mkrugenzi wa Itifaki, Mawasiliano na Mambo ya Nje Chadema, John Mrema, amezitaja kanda hizo kuwa ni za Kaskazini, Victoria, Serengeti na Kati.
Mrema amesema maandamano hayo yatakuwa na misafara miwili, itakayoongozwa na Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe na Makamu Mwenyekiti wa chama hicho bara, Tundu Lissu.
Amesema msafara wa Mbowe utaanza tarehe 22 Aprili 2024, Kanda ya Victoria mkoani Kagera, kisha siku inayofuata msafara huo utaongoza maandamano ya mkoani Shinyanga.
Tarehe 24 Aprili 2024, Mbowe na msafara wake utaongoza maandamano ya Geita Mjini. Msafara huo utahimisha maandamano hayo tarehe 30 Aprili mwaka huu, mkoani Kilimanjaro.
Msafara wa Lissu utaanzia Kanda ya Kaskazini jijini Arusha, Kisha kuhitimishwa Kanda ya Kati mkoani Morogoro.
Mrema amesema ajenda zitakazoteka maandamano hayo ni ugumu wa maisha, kikokotoo Cha mafao ya wastaafu, madai ya katiba mpya na tume huru ya uchaguzi.
Katika awamu ya pili Chadema kimepanga kufanya maandamano katika Kanda zote, wakati awamu ya kwanza yalifanyika katika majiji ya Mbeya, Mwanza, Arusha na Dar es Salaam.
Leave a comment