CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimesema marekebisho madogo ya katiba yatafanyika ili kuondoa vipengele vinavyokwamisha upatikanaji wa uchaguzi huru na wa haki.Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 22 Agosti 2023, jijini Dar es Salaam na Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara, Abdulrahman Kinana, katika mkutano ulioandaliwa na Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD), kwa ajili ya kuangalia hali ya demokrasia kuelekea chaguzi zijazo.
Baada ya baadhi ya vyama vya siasa kukosoa marekebisho ya sheria za uchaguzi kutokwenda sambamba na marekebisho ya katiba.
“Nadhani sikusema kwamba mabadiliko kwenye katiba yasifanyike, kwa wale mliokuwa bungeni 2010/15 wakati mchakato unajadiliwa ikafika mahali ukakwama 2014 bungeni. Baadae baadhi ya vyama walitoka na mapendekezo tufanye marekebisho madogo kwa ajili ya kufanya marekebisho ya uchaguzi na nilikuwa katibu nilipeleka mapendekezo wa Rais Kikwete, bahati mbaya tukashinfwa kuelewana” amesema Kinana.
Kinana amesema “…hata sasa tukitaka kufanya mabadiliko yote haya na yakagusa katiba na kama dhamira njema ipo mabadiliko yatafanywa na yataletwa marekebisho yote yanayohusu uchaguzi.”
Katika hatua nyingine, Kinana amesema kutokana na utashi na dhamira ya Rais Samia Suluhu Hassa, chaguzi zijazo zitakuwa za huru na haki.
“Rais katoa kauli nyingi juu ya kuwa na uchaguzi huru na haki na mara nyingi amekuwa akisema hakuna chama chenye hati miliki ya nchi hii, naamini tutakwenda uchaguzi ujao tukiwa na muafaka wa ujumla na maelewano yanayokiudhi kuwa na uchaguzi huru na haki,” amesema Kinana.
Awali, Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), John Mnyika, alisema mchakato wa marekebisho ya sheria za uchaguzi unapaswa uende sambamba na marekebisho ya katiba.
Amesema katiba ni muhimu kurekebishwa ili kuondoa vipengele vinavyolalamikiwa ikiwemo matokeo ya urais kutokupingwa mahakamani na zuio la mgombea binafsi.
“Tunapaswa mara baada ya kupitishwa sheria ya kuendeleza mchakato wa katiba, katika vyombo vya awali vitakavyoundwa na mchakato huo vianze na mifumo na taratibu za uchaguzi huru na haki . Maeneo ya kiuchaguzi haraka sana ifanyike marekebisho katika katiba na sio tume huru peke yake, amesema Mnyika.
“Mnyika ameshauri muswada wa kukamilisha mchakato wa katiba uwasilishwe haraka bungeni, ili kuokoa muda “sababu maoni yako tayari ili mkutano wa Bunge wa Septemba muswada upelekwe bungeni kuendeleza mchakato wa katiba ambao utajibu matatizo ambayo yanafahamika tayari.”
Mnyika amedai kuwa, katiba ya sasa ina muundo wa chama kimoja, inampa madaraka makubwa Rais, pamoja na kutotoa uhuru wa mihimili mingine ya nchi, Bunge na mahakama, vitendo alivyodai kuwa vinaminya demokrasia nchini.
Naye Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF),Mafta Nachuma, amesema kama dosari za uchaguzi zilizoibuka katika Uchaguzi Mkuu wa 2020 hazitafanyiwa kazi, uchaguzi mkuu ujao hautakuwa huru na haki.
“Tukiendelea na mfumo tulionao uliopelekea kuharibu uchaguzi wa 2020, kwa kweli hii nchi itaelekea pabaya,” amesema Nachuma.
“Sisis ACT-Wazalendo tumejitahidi kuona kwamba, lile la maridhiano na kubadilisha katiba na sheria ya uchaguzi, zibadilishwe ziwe taasisi zinazotulinda kufanya hizo demokrasia. Sasa bado chama chetu kinahimiza angalau 2023 zimalize ili tukiingia 2024 tuingie uchaguzi wa serikali za mitaa tukiwa huru na tuchague watu tunaowataka watuwakilishe,” amesema Haji.
Leave a comment