VIKAO vya Bunge, vilivyoanza mwishoni mwa Januari 2024, vimeahirishwa hadi tarehe 2 Aprili mwaka huu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Ahirisho hilo limetangazwa leo tarehe 16 Februari 2024 na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, akihitimisha shughuli za mkutano wa 14 wa Bunge la 12, bungeni jijini Dodoma.
Waziri Majaliwa amesema katika mkutano huo, maswali ya msingi 224 na mengine 871 ya nyongeza yaliulizwa na wabunge kisha kujibiwa na serikali. Maswali 12 yaliulizwa kwa Waziri Mkuu na kujibiwa katika kipindi cha maswali ya papo kwa papo.
Katika mkutano huo, miswada minne ya sheria ilipitishwa na Bunge, ukiwemo Muswada wa Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani wa 2023. Muswada wa Sheria ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi wa 2023 na Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Siasa wa 2023.
“Katika mkutano huu Bunge limeweza kutoa maazimio, azimio la Bunge ambalo limeweza kuondoa kigezo cha kupitia JKT na JKU kama sifa ya msingi ya kuweza kujiunga na vyombo vya ulinzi na usalama. Kupokea miswada minne ambayo imepitishwa kwa hatua zote,” amesema Waziri Majaliwa.
Shughuli nyingine zilizofanyika ni Bunge kujadili taarifa 16 za kamati zake, ikiwemo Kamati za Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini. Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii. Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo.
Leave a comment