KIONGOZI wa Harakati za nguvu za umma na Rais wa chama cha National Unit Platform (NUP), Robert Kyagulanyi Ssentamu amesema alishinda urais katika uchaguzi mkuu wan chi hiyo kwa asilimia 53.9 ya kura zilizopigwa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Kyangulanyi ameyasema hayo leo Jumatano tareh 11 Mei 2022 akitoa salamu za watu wa Uganda katika mkutano wa Baraza Kuu la Chadema unaofanyika jijini Dar es Salaam.
Museveni alitangazwa kuwa mshindi katika uchaguzi wa rais uliofanyika nchini Uganda 2021 akipata asilimia 58.6 ya kura zote huku Bobi Wine akitangazwa nafasi ya pili akiwa na asilimia 34.8.
“Sitaacha kuwajulisha kwamba mimi ndiye Rais niliyechaguliwa na wananchi wa Uganda,” amesema Kyangulanyi.
Amesema uchaguzi uliendeshwa huku intaneti, redio, televisheni vilizimwa na uchaguzi ambao baada yake aliwekwa kizuizini kwa siku 10 ndani ya nyumba.
Kiongozi huyo ambaye pia ni mwanamuzi anayefahamika kama Bob Wine mmesema pamoja na hayo yote huo ndio uchaguzi ambao wanachi wa Uganda walishinda.
“Pamoja na yote niliyoyataja, pamoja na mateso, vurugu na udanganyifu kwenye uchaguzi nina furaha kuijulisha dunia kuwa kwa mujibu wa taarifa za ndani ya tume nilishinda uchaguzi kwa asilimia 53.9,” amesema na kusema: “Hiyo ndiyo nguvu ya umma,”
Amesema mazingira ya siasa ya Uganda na Tanzani hayatofautiani na hata changamoto wanazopitia Uganda zipo pia Tanzania na kwa Chama.
“Sisi ni kitu kimoja, kama ilivyo hapa Tanzania tunakutana kwaajili ya mkutano mkuu baada ya uchaguzi wa mwaka 2020 na baada ya uchaguzi huo viongozi wa Chadema walikamatwa, kuteswa na baadhi yao kuuliwa,” amesema.
“Hizo ni sawa na changamoto hata sisi tunakumbana nazo na hivyo tunatakiwa kushirikiana kuhakikisha tunapambana kuleta mageuzi katika nchi zetu.”
Amesema wanajua Chadema inaelewa yale ambayo wanapitia na wapo tayari kusimama kwa pamoja kukabili changamoto hizo.
Ameongeza kuwa aliwaambia wananchi wa Uganda wakati akianza kampeni kuwa “umefika wakati wa kuachana na malalamiko na ni wakati wa vitendo.”
Amesema walichagua tumaini dhidi ya mateso wanayopitia na wameamua kuwa hawatapoteza na kwamba watashinda ama watajifunza.
Kwa kujua changamoto zetu zinafanana tumeamua kutengeneza umoja na maunganiko kupambana pamoja kama ambavyo imewahi kufanyika huko nyuma inabidi tuanze kupigania uhuru katika nchi zetu si tu Tanzania na Uganda bali Afrika kwa ujumla.
Amesema uzoefu unaonesha pale panapokuwa na changamoto jambo la kwanza la kufanya ni kuungana katika kulikabili.
Akitolea mfano wakati wa ukoloni na kupigania uhuru viongozi waliungana na walishinda na hivyo si bahati mbaya kwamba walivyoungana walishinda.
“Ushahidi ni namna nchi zetu zilivyofuatana kupata uhuru Tanzania 1961, Uganda 1962 na Kenya mwaka 1963,” amesema.
Leave a comment