MWENYEKITI wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere, Joseph Butiku ametoa wito kwa vijana nchini kutokubali kudanganyika na kujihusisha na vitendo vya uvunjifu wa amani badala yake wajiwekeze katika kufanya kazi kwa bidii ili kujiletea maendeleo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Butiku ametoa wito huo leo tarehe 11 Mei, 2022 jijini Dar es Salaam wakati akizungumza katika uzinduzi wa mradi wa VijanaNaAmani255 ulioratibiwa na Shirika la Global Peace Foundation (GPF).
Mradi huo unalenga kutoa elimu kwa vijana mashuleni juu ya ujenzi wa amani kwa kushirikiana na Chama cha Skauti Tanzania.
Pia kufikisha elimu ya ujenzi wa amani kwa makundi mbalimbali ya vijana na jamii kwa ujumla kupitia warsha mbalimbali na uelimishaji kwa njia ya mtandao ili kukuza ushiriki wa vijana katika ujenzi wa amani.
Kutokana na ujio wa mradi huo, Mzee Butiku amewaasa vijana kutambua kuwa ni muhimu kuitunza amani kwani matokeo ya amani kwa jambo lolote ni maendeleo.
“Katika utu wetu hakuna mtu aliye na thamani zaidi ya mwingine, hivyo ili kutambua hili ni lazima kuilinda amani ili kila mtu afanye kazi na kupata mahitaji yake muhimu kama binadamu,” amesema.
Aidha, akifafanua kuhusu ‘Vijana Na Amani255’, Mratibu wa Mradi huo, Joseph Malekela amesema mradi pia utatekelezwa kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Taasisi za Mwalimu Nyerere Foundation, Youth of United Nations Association (YUNA) na Global Religious for Children Foundation – GRCF).
Amesema mradi wa #VijanaNaAmani255 unatarajiwa kutekelezwa kuanzia Mei mwaka huu hadi Mei 2024.
Amesema kwa upande wa shughuli za mitandaoni wanatarajia kuhamasisha vijana kushiriki katika ujenzi wa amani, kuwa mabalozi wa amani kwenye jamii, kuepuka vurugu, kupinga kauli za chuki na taarifa za uongo sambamba na kusambaza jumbe zinazolenga kukuza amani, upendo na mshikamano kwenye jamii.
“Hii yote ni kupitia mijadala itakayoandaliwa kwa njia ya mitandao ambayo vijana watapata nafasi ya kushiriki, kujifunza na kujadili.
“Shughuli za ana kwa ana, tunatarajia kuwafikia vijana mashuleni, vijana walio katika makundi yenye ushawishi katika jamii, viongozi wa dini na wafanya maamuzi katika ngazi mbalimbali za jamii ili kwa kujadili namna ya kukuza ushiriki na ushirikishwaji wa vijana kwenye suala zima la ujenzi wa amani, ulinzi na usalama,” amesema.
Aidha, Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Global Peace Foundation (GPF), Martha Nghambi amesema mradi huo unalenga kufikia mikoa ya pembezoni ambapo kwa hatua ya awali, wanatarajia kutekeleza mradi wa #VijanaNaAmani255 katika mikoa mitatu.
“Tutekeleza katika mkoa wa Lindi (Wilaya za Kilwa na Nachingwea), Mtwara (Wilaya za Mtwara na Tandahimba) na Ruvuma (Wilaya za Tunduru na Nyasa) kwa uwezeshaji wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa – UNDP,” amesema.
Aidha, akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkazi wa UNDP nchini, Christine Musisi, Ofisa miradi wa shirika hilo nchini, Sofia Chehbouni amesema wanaamini mradi huo utahimiza jamii ya kitanzania kudumisha amani, upendo na mashikamano ili Tanzania izidi kusonga mbele zaidi.
Hata hivyo, akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Prof. Joyce Ndalichako, Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Vijana Ofisi ya Waziri Mkuu, Julius Tweneshe ametoa wito kwa vijana kuchangamkia fursa zinazotolewa na ofisi hiyo.
Ametaja fursa hizo kuwa ni ruzuku kutoka katika mfuko wa maalumu uliopo chini ya wizara hiyo pamoja na mikopo inayotolewa na halmashauri zote nchini.
Tweneshe ambaye alikuwa mgeni rasmi kwa niaba ya Prof. Ndalicho amesema vijana wakijishughulisha na kazi hakutakuwa na makundi ya uhalifu kama inavyotokea sasa jijini Dar es Salaam kwa ‘Panya road’.
Naye Balozi wa vijana katika ujenzi wa amani ndani ya Afrika Mashariki, Eben Mnzava, Eben Mnzava amesema mradi huo umekuja wakati muafaka hasa ikizingatiwa Tanzania ni mojawapo ya nchi zinazoathiriwa na matukio ya uhalifu kwa asilimia asilimia tano Afrika Mashariki.
Shirika la Global Peace Foundation Tanzania ni taasisi isiyo ya kidini, kibiashara, Kiserikali wala kisiasa inayojishughulisha na uhamasishaji wa jamii kuishi kwa amani na utulivu.
GPF inatoa mafunzo ya kuwawezesha wanawake na vijana kiuchumi, kiuongozi, kujitambua, kujitegemea, na kuhamasisha matumizi mazuri ya mitandao ya kijamii ili kudumisha amani.
Leave a comment