MAMLAKA ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura) imetangaza bei mpya za nishati ya mafuta nchini ambazo zimeanza kutumika leo Novemba 1, 2023 huku katika mikoa ya Dar es Salaam, Tanga na Mtwara, mafuta ya petrol na dizeli zikionekana kushuka ilihali mafuta ya taa yakipanda. Anaripoti Mwandishi Wetu… (endelea).
Kwa mujibu wa tangazo hilo la Ewura katika mkoa wa Dar es Salaam, lita mmoja ya Petroli kwa bei ya rejareja itauzwa Sh 3,274, dizeli ni Sh 3,374 na mafuta ya taa yatauzwa kwa Sh 3,423.
Kutokana na tangazo hilo la bei hizo mpya, inaonyeshakuwa petrol imeshuka kwa Sh7 kwa lita wakati dizeli imeshuka kwa Sh74 kwa lita, huku mafuta ya taa yakipanda kwa Sh480 kwa lita, tofauti na bei kikomo zilizotangazwa mwezi uliopita kwa mkoa wa Dar es Salaam.
Katika mkoa wa Tanga, petroli itauzwa kwa Sh3,274 kutoka Sh3,327, huku dizeli ikiwa imepanda kutoka Sh3,494 hadi Sh3,510; na mafuta ya taa yatauzwa Sh3,469 tofauti na ilivyokuwa mwezi uliopita ambapo yaliuzwa Sh2,989.
Kwa upande wa mkoa Mtwara, petroli itauzwa Sh3, 347, dizeli Sh3,546, mafuta ya taa yamepanda kutoka Sh3,016 had Sh3,495.
Ewura imesema mabadiliko ya bei za mafuta kwa mwezi Oktoba 2023 yanatokana na kupungua kwa bei za mafuta katika soko la dunia kwa wastani wa asilimia 5.68 na gharama za uagizaji wa mafuta kwa wastani wa asilimia 13 kwa petroli, asilimia 25 kwa dizeli na uamuzi wa wazalishaji wakubwa wa mafuta duniani (OPEC+) kupunguza uzalishaji na vikwazo vya kiuchumi ambavyo nchi ya Urusi imewekewa.
Aidha, imesisitiza wafanyabiashara wa bidhaa za mafuta kwa rejareja wanatakiwa kuuza mafuta kwa bei zilizotangazwa na mamlaka hiyo.
Leave a comment