WAZIRI wa Ujenzi, Innocent Bashungwa ameahidi kuendelea kudumisha ushirikiano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika sekta ya ujenzi ili uboreshaji wa miundombinu ya ujenzi upatikane katika maeneo yote ya bara na visiwani. Anaripoti Danson Kaijage, Mwanza (endelea).
Bashungwa ametoa kauli hiyo jana jijini Mwanza katika mkutano wa sita wa sekta hiyo uliobeba kauli mbiu ya “Ushirikiano imara kwa miundombinu na muungano imara”.
Pia ameahidi kusimamia kwa karibu mapendekezo na maazimio yote waliyokubaliana katika mikutano inayofanyika kwa faida ya pande zote mbili za muungano.
Aidha, Bashungwa amempongeza Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Dk. Hussein Mwinyi kwa kutimiza miaka mitatu tangu aingie madarakani.
Amesema katika kipindi hicho kumekuwa na mageuzi makubwa kwenye sekta ya ujenzi ambayo ni kichocheo kikubwa katika ukuaji wa sekta ya utalii, elimu na afya na hivyo kukuza uchumi wa Taifa kiujumla.
Naye Mwenyekiti mwenza kutoka Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi (SMZ), Dk. Khalid Mohamed amesema kwa kuzingatia kazi za Serikali inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan na Rais wa Zanzibar Dk. Hussein Mwinyi, sekta ya ujenzi imepiga hatua kubwa ya kimaendeleo kwa Tanzania Bara na Zanzibar.
Amesema miundombinu katika pande hizo mbili imeshamiri na hivyo kuchochea ukuaji wa utalii na hivyo kukuza uchumi wa taifa.
“Kwa kipindi cha miaka mitatu cha uongozi wa Rais Dk. Mwinyi tumepata mafanikio makubwa katika ujenzi wa miundombinu ya barabara za Mijini na Vijijini ambapo zaidi ya kilomita 846 za barabara zinaendelea kujengwa Unguja na Pemba kwenye mtandao wa barabara wenye takribani kilometa 1,344”, amesema Dkt. Mohamed.
Leave a comment