ALICIA Magabe, mke wa mgombea urais wa Tanzania kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu, ameeleza jinsi walivyokutana na kukubaliana kisha kufunga ndoa. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Alicia alitoa simulizi hiyo jana Ijumaa tarehe 4 Septemba 2020 katika mkutano uzinduzi wa kampeni Kanda ya Kati inayohusisha mikoa ya Singida, Dodoma na Morogoro zilizofanyika Uwanja wa Shule ya Msingi Uhuru jijini Dodoma uliofanywa na Lissu.
Akimwombea kura Lissu katika mkutano huo, Alicia alisema, ana kila sababu ya kumshukuru Mungu na Wanadodoma kwani mara ya mwisho aliondoka Dodoma yeye (Alicia) akiwa na Lissu aliyekuwa mahututi.
Tarehe 7 Septemba 2017, Lissu alishambuliwa kwa risasi zaidi ya 30 na watu wasiojulikana akiwa anataka kushuka katika gari nyumbani kwake Area D jijini Dodoma akitoka kuhudhuria kikao cha Bunge.
Baada ya kushambuliwa, alipelekwa Hospitali ya Rufaa ya Dodoma kwa matibabu ya awali kisha, usiku wa siku hiyohiyo alihamishiwa Hospitali ya Nairobi nchini Kenya akiwa hajitambui kutokana na shambulio hilo.
“Leo nina kila sababu ya kumshukuru Mungu, mara ya mwisho kuondoka Dodoma niliondoka na mtu (Lissu) aliyekuwa amemiminiwa risasi lakini leo nimerudi akiwa mzima na nyie mnamuona,” alisema Alicia huku akishangiliwa na umati uliojitokeza kwenye mkutano huo.
Alicia alisema “Dodoma mlikuwa wahudumu wa kwanza na mlihakikisha anapata kila msaada kutibiwa, kufika Nairobi na baada ya kwenda Ubelgiji.”
Akigusia walivyokutana, Alicia alisema “huyu baba nilimfaamu muda mrefu tukiwa jeshini na baada yake kitivo cha sheria lakini nilivutiwa naye sana japo nilikuwa nadengua dengua kwanza.”
Huku shangwe zikitawala uwanjani hapo, Alicia alisema “nilivutiwa naye kwa msimamo wake wa kutetea watu, msimamo wake na hata aliposema anarudi nyumbani nilikuwa na hofu lakini leo anaweza kusimama na kumuombea kura.”
“Naomba sana wa Dodoma wake kwa waume, naomba mmpe kura kwani naamini atakuwa Rais bora wa kuwatetea watu wote na kuondokana na uonevu” alisema Alicia waliyebahatika kupata watoto wawili mapacha wa kiume na Lissu.
Leave a comment