MGOMBEA ubunge wa Ubungo, Dar es Salaam kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Profesa Kitila Mkumbo amesema, akichagulia atahakikisha anaishaiwi Serikali kujengwa ukumbi wa kisasa wa michezo (Sports Arena) ndani ya jimbo hilo. Anaripoti Hanisi Mguta, Ubungo … (endelea).
Profesa Mkumbo ametoa ahadi hiyo leo Ijumaa tarehe 4 Septemba 2020 wakati akizindua kampeni za uchaguzi wa jimbo hilo katika uwanja wa EPZA Ubungo External.
Uchaguzi Mkuu wa madiwani, wabunge na Rais wa Tanzania utafanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020.
Kampeni za uchaguzi huo zimekwisha kuanza tangu tarehe 26 Agosti na zitahitimishwa 27 Oktoba 2020.
Akizungumza katika mkutano huo wa kampeni, Profesa Mkumbo amesema, jimbo la Ubungo limebarikiwa kuwa na mabondia wengi maeneo ya Manzese, Ubungo na Mabibo ambao ni mchezo unaopaswa kupewa kipaumbele kwani unachangia ajira na pato la Taifa.
“Leo nilikuwa nazungumza na bondia maarufu nchini Mfaume Mfaume. Nikamuuliza niambie jambo moja ambalo kama ukipata nafasi ya kukutana na Rais John Magufuli utamweleza aitendele sekta ya michezo.”
“Akaniambia tujenge Arena ambayo ndani kuna kila kitu, kama eneo la kuchezia ngumi, ukumbi wa burudani na jambo hili limenigusa sana kama mtanichagua nitakwenda kumshauri Rais ili kujenga Arena Ubungo,” amesema Profesa Mkumbo
Mhadhiri huyo wa zamani wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) amesema, nchi ya Rwanda ambayo kwa ukubwa haiifikii Tanzania, yenyewe tayari ina ukumbi wa kisasa wa michezo (Sports Arena) kwa hiyo “nchi kubwa kama Tanzania lazima tuwe na Arena na hili nitaisimamia ili tujenge Ubungo.”
Profesa Mkumbo amesema “Tukiwa na Arena italeta fursa ya ajira kwa vijana na ninaomba mtupe nafasi ya kuongoza ili nikashawishi hili.”
Amesema, kujengwa kwa ukumbi huo utawezesha kufanyika matamasha makubwa ya wasanii jambo litakalovutia wasanii wengi wa nje kuja Tanzania.
Leave a comment