KATIBU Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo, Ado Shaibu, amesema chama chake kitaanza kuisimamia Serikali katika majimbo yote nchini, ili kuhakikisha kero za wananchi zinatatuliwa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Ruvuma … (endelea).
Ado ametoa kauli hiyo leo Jumatano, tarehe 5 Oktoba 2022, katika ziara yake Kata ya Ligunga, wilayani Tunduru, Mkoa wa Ruvuma, baada ya baadhi ya wananchi wa wilaya hiyo kuibua changamoto sugu zinazowakabili.
“Tunduru sitowaacha. Tunafahamu kuwa madiwani na wabunge hawawajibiki kushughulikia kero zenu. Nimezunguka Tunduru Kusini na Kaskazini, kote kumejaa kero ambazo zinapaswa kufuatiliwa. Inasikitisha kuwa wabunge wa hapa wameamua kuwa mabubu Bungeni,” amesema Ado.
Miongoni mwa changamoto ambazo Ado amedai zinawakabili wananchi hao ambazo hazijafanyiwa kazi, ni uvamizi wa wanyamapori, katika makazi ya watu uliosababisha baadhi yao kupoteza maisha.
“Mimi na Mtutura (aliyekuwa Mgombea Jimbo la Tunduru Kusini), tutakuwa Wabunge wa Nje ya Bunge. Tutapaza sauti dhidi ya mauaji yanayofanywa na tembo, stakabadhi ghalani, uingizwaji holela wa Ng’ombe na kupigania huduma nzuri za kijamii kwa Wanatunduru”-alisisitiza Ndugu Ado na kuongeza:
“Utaratibu huu utakuwa kwa majimbo yote Nchini. Tutaweka utaratibu wa kuwa na sauti Nje ya Bunge ya kuwasemea wananchi. Lengo letu ni kuwa sauti mbadala ya uhakika kwa wananchi.”
Leave a comment