Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelenskyy amesema zaidi ya wanajeshi 31,000 wamefariki vitani katika muda wa miaka miwili tangu Urusi ilipoivamia Ukraine. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Kutokana na hali hiyo, Rais Zelensky amesema ushindi wa nchi yake unategemea uungwaji mkono wa nchi za Magharibi.
Kiongozi huyo ameeleza matumaini yake kuwa Marekani itaidhinisha kifurushi cha msaada muhimu wa kijeshi kwa Ukraine.
Zelensky pia ameongeza kwamba Urusi inapanga kufanya mashambulizi zaidi katika msimu ujao wa joto.
“Tutajiandaa kwa shambulio hilo. Mashambulizi yao walioyafanya tangu tarehe 8 Oktoba mwaka jana hayakuwa na matokeo yoyote, hilo naamini. Sisi kwa upande wetu, tutaweka mipango madhubuti na kuifuata,” ameeleza Zelensky.
Ametoa wito kwa nchi za Magharibi kuiunga mkono Ukraine kwa dhati ili kuipa nafasi ya ushindi katika kumbukumbu ya miaka miwili ya uvamizi wa vikosi vya Urusi.
Katika wiki za hivi karibuni, wanajeshi wa Ukraine wamekabiliwa na uhaba wa risasi na makombora, baada ya mzozo katika bunge la Marekani kuhusu msaada wa kijeshi wa dola za Marekani bilioni 60 kwa Kiev.
Wiki iliyopita, wanajeshi hao walilazimika kuondoka katika mji wa mashariki wa Avdiivka katika jimbo la Donestk ambako hali inaripotiwa kuwa mbaya.
Leave a comment