RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, amewataka wananchi washiriki katika zoezi la kutoa maoni kwa ajili ya maandalizi ya Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050, linaloendelea nchi nzima. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar…(endelea).
Mkuu huyo wa nchi, ametoa wito huo leo tarehe 31 Agosti 2023, akifunga Tamasha la Kizimkazi la mwaka huu, visiwani Zanzibar.
“Nitoe wito wa kuwataka wananchi wote kushiriki kikamilifu katika kutoa maoni kwa ajili ya maandalizi ya Dira ya Maendeleo ya Taifa letu ya 2050. Kama mnavyojua dira yetu inaishia 2025 na sasa Wizara ya Mipango na Uwekezaji, wakishirikiana na Wizara ya Fedha, wameanza maandalizi ya dira ya 2050 ambayo tumeanza kuchukua maoni. Nawaomba mshiriki kikamilifu,” amesema Rais Samia.
Mbali na hayo, Rais Samia amewataka wadau wa maendeleo kushirikiana na Serikali katika utekelezaji wa Mradi wa Jenga Kesho Bora kwa Vijana (BBT), unaolenga kutatua changamoto za ajira, huku akibainisha kwamba mradi huo utahusisha Tanzania Bara na Zanzibar.
“Mradi huu hautaishia kule Tanzania Bara, lakini ni mradi wa Tanzania nzima, sasa hapa Kusini mmeona vijana wengi wamepita na fursa nyingi zipo baharini, vijana hawa wanaweza fanya shughuli nyingi ndani ya bahari na tukaweza kuwajengea kesho iliyo bora,” amesema Rais Samia.
Akizungumzia tamasha hilo, Rais Samia amesema limelenga kuimarisha maadili ya watoto kwa kuonyesha tamaduni mbalimbali ili wazirithi.
“Tamasha la mwaka huu kauli mbiu yake ni kuwalinda kimaadili watoto wetu kwa maslahi ya taifa. Hii ni kauli mbiu muafaka kabisa na tukitaka kudumisha utamaduni, mila na desturi zetu hatuna budi kuhakikisha tamaduni na mila hizo zinarithishwa kwa watoto wetu,” amesema Rais Samia.
Mbali na tamasha hilo kuenzi tamaduni, Rais Samia amesema linachochea maendeleo kwa kuwa baadhi ya miradi imefunguliwa huku mingine ikiwekewa jiwe la msingi, wakati likifanyika.
Leave a comment