KAMPUNI ya Transworld Aviation Dubai, kutoka Falme za Kiarabu, imeomba Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), kuiondolea zuio la kufanya kazi katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume, kituo cha Terminal III, Kwa kuwa linakiuka mkataba wa uwekezaji. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Ombi Hilo limetolewa tarehe 4 January 2022 na Mkurugenzi wa Sheria na Uwekezaji was Kampuni ya Transworld Aviation Dubai, Peter Madeleka, akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam.
Wakili Madeleka amesema, kampuni hiyo iliingia mkataba wa miaka 15 na SMZ, kupitia Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TCAA), ambao unaelekeza wafanye kazi katika uwanja wote bila kubagua, lakini katazo linaifanya kuhudumia maeneo ambayo ndege za ndani zinatua, badala ya maeneo ambayo ndege za kimataifa zinatua.
Madeleka amesema, katazo hilo linaathiri utendaji wa kampuni hiyo kwa kuwa linashindwa kuhudumia wateja wake wa kimataifa ambao wanatumia uwanja huo.
Ametaja baadhi ya wateja wake kuwa ni NEOS SPA ya Italia, Kenya Airways ya Kenya, Astral Aviation ya Kenya Fly Dubai, KLM ya Uholanzi.
Amedai kuwa, katazo hilo ni la kibaguzi kwa kuwa kampuni moja aliyoitaja kwa jina la Dnata Zanzibar Aviation Services Company Limited, imepewa ruhusa ya kufanya kazi peke yake katika kituo hicho.
Aidha, Madeleka amesema SMZ imetoa katazo hilo kupitia Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Zanzibar (ZAA), bila kuishirikisha kampuni ya Transworld Aviation Dubai, kupitia kampuni yake dada Transworld Zanzibar, pamoja na kutotaja sababu zenye tija zilizopelekea kuchukua uamuzi huo.
“Changamoto hii inakwenda kuharibu mahusiano yaliyopo na kusababisha hasara kutokana na uwekezaji tulioufanya, Hilo katazo ni kinyume na mkataba. Sisi tulikuwa na wateja wetu ambao ni ndege za kimataifa, Hilo katazo halizingatii masharti ya mkataba tulio nao sababu wateja wetu wanatua terminal three sisi watoa huduma haturuhusiwi kwenda,” amesema Madeleka.
Madeleka ameitaka SMZ kuilipa fidia kampuni hiyo kiasi Cha Sh. 540 milioni kutokana na hasara iliyopata kwa kushindwa kufanya kazi katika Terminal III tangu Desemba mwaka Jana, huku akidai wateja wake wametishia kuvunja mkataba kutokana na kukosa huduma kwenye uwanja huo.
Amesema, kama SMZ isipochukua hatua kushughulikia suala hilo kampuni hiyo itakwenda katika Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Migogoro ya Kibiashara, kwa ajili ya kupata suluhu.
“Tumefanya juhudi kuwasiliana na mamlaka wamesema wanashughulikia na wanatuambia liko wizarani. Kama wasipotafuta sukuhu tunakwenda mahakama ya usuluhishi wa migogoro ya kibiashara ambalo tumekubaliana mahakama hiyo itatoa tafsiri sahihi ya namna ganu itapaswa kuwa lakini hatutarajii kufiksha huko sababu suala hili linazungumzia,” amesema Madeleka.
Alipotafutwa Mkurugenzi wa TCAA, Hamza Johari kupata ufafanuzi zaidi wa suala hilo, alisema liko chini ya ZAA, hivyo wao ndiyo wenye mamlaka ya kulitatua.
Jana MwanaHALISI Online ilimtafuta Mkurugenzi Mkuu wa ZAA,Seif Abdallah, kwa ajili ya taarifa zaidi, alisema madai hayo hayana ukweli, alipoulizwa zaidi kuhusu suala hilo alijibu yuko kwenye kikao apigigiwe baadae hata hivyo baadae alipotafutwa hakupokea simu.
Leave a comment