SERIKALI ya Tanzania, imewaita wadau wa Asasi za Kiraia kutoa maoni yao juu ya maboresho ya rasimu ya mpango kazi wa pili wa taifa wa haki za binadamu (2021-2026). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Wito huo umetolewa leo Jumanne, tarehe 10 Mei 2022, jijini Dar es Salaam na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Dk. Khatibu Kazungu, katika kikao cha wadau wa haki za binadamu kwa ajili ya kuhakiki rasimu hiyo.
Kikao hicho kimeandaliwa na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), na kuhudhuriwa na wanachama kutoka asasi za kiraia mbalimbali.
“Ni matarajio yangu kwamba mtaweza kuwasilisha michango yao juu ya namna ya kuboresha rasimu ya mpango kazi. Naamini baada ya kupitia rasimu iliyopo mtatoa michango yenu kikamilifu kwa kuwa mchakato unaendelea zoezi hili ni muhimu kuhakikisha Serikali inakamilisha wajibu wake wa kukuza na kulinda haki za binadamu,” amesema Dk. Kazungu.
Dk. Kazungu amesema rasimu hiyo umezingatia masuala mbalimbali yanayohusu haki za binadamu na watu Tanzania, ikiwemo haki za kiraia na kisiasa, haki za kiuchumi na utamaduni na haki za makundi maalumu.
“Moja ya haki za kiraia na kisiasa, yafuatayo yamezingatiwa ikiwemo upatikanaji wa haki na usawa mbele ya sheria, uhuru wa mawazo na kujieleza na kupata taarifa. Kwenye haki za kiuchumi, utamaduni na kijamii, imezingatia haki ya kupata maendeleo na kuishi kwenye mazingira safi na salama,” amesema Dk. Kazungu.
Kwa upande wake Mratibu wa THRDC, Onesmo Olengurumwa, amesema asasi za kiraia zitaendelea kutoa ushirikiano wake kwa Serikali, katika uimarishaji haki za binadamu.
“Mchakato huu unazingatia hatua tano,hatua ya kuoata maoni na uandaaji, ufuatiliaji, utekelezaji na hatua ya kufanya tathmini na yote hii asasi tumekuwa wadau wanaosimamia utekelezaji haki hizo.
“Asasi tupo pamoja na Serikali yetu na tutaendelea kuendeleza ushirikiano,” amesema Olengurumwa.
Leave a comment