RAIS Samia Suluhu Hassan ametangaza kuanzishwa kwa kombe la mashindano ya utamaduni nchini katika matamasha yajayo yatakayohusisha makabila yote nchni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mwanza … (endelea).
Rais Samia ametoa kauli hiyo leo tarehe 8 Septemba mwaka huu wakati akihutubia katika Tamasha la Utamaduni, Mila na Desturi zetu lililofanyika Viwanja vya Red Cross Kisesa jijini Mwanza.
Amesema kwa kuwa Tanzania inayo makabila zaidi ya 120, ni vema katika matamasha yajayo machifu na watemi kujipanga ili kushinda kombe hilo.
Amesema lengo la mashindano hayo ni kuendelea kuutangaza utamaduni wa watanzania kama ilivyo kwa nchi za Ethiopia na Indonesia ambazo zinaingiza pato la kutosha katika kutangaza utamaduni wao pekee.
Amesema kwa upande wa Tanzania, Serikali ilikuwa imewekeza kutangaza utalii wa vivutio kama vile wanyama na milima na kusahau utamaduni ambao pia ni kivutio cha kipekee.
Aidha, amewaahidi kufanyia kazi baadhi ya changamoto ambazo Umoja wa Machifu Tanzania wamemuomba ikiwa ni pamoja na kutambuliwa, kupoteza himaya za maeneo yao ya utamaduni na baadhi ya majengo.
“Najua sijakutana nanyi kama makundi mengine nilivyopanga kukutana nayo, ila changamoto zote nimezipokea.
“Pamoja na hayo ninawaombe muendelee kuchukua tadhahari kuhusu ugonjwa wa corona lakini pia kwa kuwa mwakani tunaanza sensa, ninaomba mtoe ushirikiano wa kutosha kwa maofisa wetu kwa lengo la kupata takwimu sahihi,” alisema.
Leave a comment